KIONGOZI mpya wa kijeshi wa Burkina Faso ameahidi kurejea kwa utaratibu wa kawaida wa kikatiba wakati hali itakapokuwa sawa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Luteni Kanali Paul-Henri Damiba aliongoza mapinduzi yaliyomuondoa madarakani Rais wa nchi hiyo, Roch Kaboré tarehe 24 Januari, 2022.
Katika hotuba yake jana tarehe 27 Januari, 2022, alimlaumu rais huyo kwa kushindwa kuzuia ghasia za wanamgambo wa Kiislamu.
Akiwa amevalia kofia nyekundu na mavazi ya kijeshi, Luteni Kanali Damiba alihutubia taifa kwa mara ya kwanza kwenye televisheni ya taifa tangu achukue mamlaka.
“Mambo yatakapokuwa sawa, kulingana na tarehe ya mwisho ambayo watu wetu watafafanua katika mamlaka yote, ninajitolea kurejesha utaratibu wa kawaida wa kikatiba,” alisema.
Luteni Kanali Damiba mwenye umri wa miaka 41, alisema atakutana na wawakilishi wa sehemu mbalimbali za jamii ili kukubaliana kuhusu mpango mageuzi.
Aliongeza kuwa Burkina Faso inahitaji washirika wa kimataifa zaidi ya hapo awali, kufuatia kulaaniwa kwa mapinduzi hayo.
“Ninatoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuunga mkono nchi yetu ili iweze kuondokana na mgogoro huu haraka iwezekanavyo.”
Jeshi lilitangaza kuwa limetwaa mamlaka kwenye televisheni ya taifa siku ya Jumatatu.
Kaboré alikabiliwa na hali ya kutoridhika iliyoongezeka kutokana na kushindwa kwake kukomesha ghasia za wanamgambo wa Kiislamu.
Luteni Kanali Damiba amekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya wanamgambo wa Kiislamu.
Aliandika kitabu juu ya mada hiyo mwaka jana.
Matatizo kama hayo katika nchi jirani ya Mali yalisababisha mapinduzi ya kijeshi mwezi Mei 2021 – ambayo yalipokelewa kwa furaha na Umma.
Burkina Faso ni nchi ya tatu ya Afrika Magharibi kushuhudia jeshi likichukua madaraka katika miaka ya hivi karibuni.
Guinea na Mali zimewekewa vikwazo na jumuiya ya kikanda ya Ecowas ili kuzishinikiza kurejea kwa utaratibu wa kikatiba.
ECOWAS inakutana leo tarehe 28 Januari, 2022 kujadili jinsi ya kushughulikia mapinduzi ya hivi karibuni katika eneo hilo.
Leave a comment