CHRISTIAN Emmanuel Sanon (63), anayedaiwa kusuka mikakati ya mauaji ya aliyekuwa Rais wa Haiti, Jovenel Moise (53), amedakwa na Jeshi la Polisi nchini humo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Taarifa hiyo ilitolewa jana tarehe 11 Julai 2021 na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini humo, Leon Charles, akielezea msako wa watu waliohusika katika mauaji ya Rais Moise, yaliyotokea tarehe 7 Julai mwaka huu, katika makazi yake binafsi, yaliyopo kwenye milima ya Prt-au-Prince.
Charles amedai kuwa, Sanon ambaye ni raia wa Haiti aishiye Florida nchini Marekani, alipanga njama za mauaji hayo kwa kuajiri kundi la mamluki wakiwemo raia wa kigeni, kwa ajili ya kumuondoa madarakani rais huyo ili apate nafasi ya kuitawala nchi hiyo.
Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi nchini Haiti, amedai miongoni mwa watu waliokuwemo katika kundi la mamluki hao, ni Raia wa Colombia 18, waliokuwa wanafanyakazi katika kampuni binafsi ya ulinzi yenye makazi yake Florida nchini Marekani.
Sanon anaungana na watuhumiwa wengine 20 walioko kizuizini, tangu tarehe 8 Julai mwaka huu, kwa tuhuma za kuhusika na tukio hilo.
Amedai kuwa, Juni 2021, mtuhumiwa huyo aliwasili nchini Haiti akiwa na walinzi wake, kwa kutumia ndege binafsi .
Inadaiwa kuwa, Askari Polisi nchini humo walimkamata Sanon nyumbani kwake, akiwa na masanduku 20 ya risasi, bunduki, namba za usajiri za gari nne tofauti, kutoka nchini Jamhuri ya Dominika na magari mawili.
Moïse, amekuwa madarakani tangu Februari 2017, baada ya mtangulizi wake, Michel Martelly kung’atuka mamlakani.
Katika kipindi hicho cha utawala wake, Moise alikuwa akikabiliwa na tuhuma za ufisadi hali iliyosababisha maandamano ya mara kwa mara ya wananchi wa kupinga uongozi wake.
Katika maandamano ya mwaka 2019 ya kumpinga, Rais Moise, alisema “hatondoka nchini kwasababu ya shinikizo kutoka kwa magenge yaliyojihami na walanguzi wa dawa za kulevya.”
Mapema mwaka 2021, maandamano yalifanyika yakimtaka kujiuzulu nafasi hiyo kutokana na tuhuma mbalimbali.
Leave a comment