MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)-Bara, Abdulrahman Kinana amewataka viongozi wa Serikali kutumia njia ya ushawishi badala ya amri, katika kuwaongoza wananchi, kwani njia hiyo huleta matokeo chanya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Pwani … (endelea).
Kinana ametoa wito huo leo Jumatano, tarehe 12 Oktoba 2022, akifungua mdahalo wa kumbukizi ya miaka 23 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, lililofanyika kwenye Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha mkoani Pwani.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, amewataka viongozi hao hasa vijana, kufuata nyayo za Mwalimu Nyerere, katika kutumia njia ya ushawishi wanapotekeleza majukumu yao.
“Mwalimu Nyerere alikuwa na maono marefu yaliyoona mbali na kila kiongozi wa ngazi yoyote pale unapopewa nafasiu kitu cha kwanza kujiuliza nimekuja kufanya nini. Hapa nataka nifanikiwe nitakapoondoka nataka nikumbukwe kwa yepi, bahati nzuri viongozi wa sasa wengi ni vijana lazima ujiulize hao unaowaongoza unawashawishi vipi?
“Si kwa kutoa amri na maelekezo lakini kwa kuwashawishi na kwenda hao. Binadamu sio wanyama wa kupewa amri na wa kuswagwa, ni wa kupewa maelekezo, kufahamishwa na kwenda nao pamoja katika safari ya kuleta maendeleo katika eneo ulilopewa dhamana ya kuongoza wenzako,” amesema Kinana.
Kinana amewakumbusha viongozi kuwa nyadhifa zao ni dhamana ambazo hazidumu, hivyo waepuke utukufu.
“Uongozi ni utumishi, ukijali sana itifaki utakuwa unajali utukufu badala ya utumishi. Kwa hiyo tuepuke utukufu na tutukuze utumishi, Ukijali sana itifaki utakuwa unajali utukufu badala ya utumishi. Kwa hiyo tuepuke,” amesema Kinana.
Leave a comment