MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), amevitaka vyama vya siasa vikubali kushiriki mikutano inayoitishwa kwa ajili ya kujadili masuala ya demokrasia, kwani ndiyo njia pekee ya kutafuta suluhu ya changamoto zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Kinana ametoa wito huo leo Jumanne, tarehe 5 Aprili 2022, jijini Dodoma, akihutubia katika kongamani la haki, amani na maridhiano lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), lililofunguliwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
Kinana amesema chama chake kiko tayari kufanya mazungumzo na vyama vingine vya siasa, kujadili masuala yanayohusu maridhiano.
“Nataka niwahakikishieni CCM itakuwa tayari kukutana na vyama vyote ili kujadiliana masuala yanayohusu maridhiano, amani pamoja na demokrasi,”
“Nivisihi vyama nianze na mimi mwenyewe, tunapiitana tukutane hata kama tuna tifauti zetu hatukubaliani kwenye mambi mengi , tukikutana polepole yale tusiyikubaliana yatapungua na hatimaye tukayapunguza kabisa,” amesema Kinana.
Kinana ametoa ujumbe huo katika kipindi ambacho Chama cha Chadema na NCCR-Mageuzi, vimesusa kushiriki kongamano hilo, wakidai kuna baadhi ya mapendekezi yao hayajafanyiwa kazi, ikiwemo la kufanyika mkutano na Rais Samia kujadili ajenda zake.
Kinana amessma “nchi ni ya vyama vingi na tumekubali kisheria, kikatiba kwamba Tanzania ni nchi ya vyama vingi. Kwa kutambua hilo nataka niwasihi wenzangu tujenge utamaduni wa kukutana vyama vyote.”
Aidha, Kinana ameahidi atakapokabidhiwa uenyekiti wa TCD na Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, ataimarisha mshikamano wa vyama vya siasa.
“Kama mwenyekiti ninayekuja, nitajitahidi kuvikutanisha vyama ili tuweze kuwa na mshikamano, tuelewane vizuri zaidi tuweze kuijenga nchi yetu,” amesema Kinana.
Mwanasiasa huyo amewahakikishia mabalozi waliohudhuria kongamano hilo kuwa, Serikali itajitahidi kuimarisha umoja wa kitaifa.
“Nashukuru mabalozi kwa heshima mliyotupa, nina hakika mnaipenda nchi hii, mnapenda kuona maendeleo ya nchi hii. Maendeleo ya nchi yanaanza na umoja wa kitaifa na sisi tungependa kufika hatua hii,” amesema Kinana.
Leave a comment