WAJUMBE wa zamani wa Bodi ya Wadhamini ya Chama cha NCCR-Mageuzi, wameendelea kupambana mahakamani kupinga uteuzi wa wajumbe wapya, wakidai ulifanyika kinyume cha Sheria. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni katika kesi ndogo Na. 570/2023 waliyofungua ndani ya kesi ya msingi Na. 150/2022, katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, kuiomba mahakama hiyo itamke wajumbe wapi halali wa bodi hiyo.
Leo Jumanne, tarehe 24 Januari 2023, mahakamani hapo mbele ya Jaji Ephery Kisanya, Wakili wa wajumbe hao wanaodaiwa kufukuzwa NCCR-Mageuzi, Hardson Mchau, ameiomba mahakama iwatambue kuwa wajumbe halali kwa kuwa mchakato wa kuwaondoa ulikwenda kinyume cha sheria na katiba ya chama hicho.
Akiwasilisha hoja za kisheria katika kesi hiyo, Wakili Mchau amedai kuwa, mchakato uliotumika kuwaondoa wajumbe hao ulikiuka haki ya asili kwa kuwa uamuzi huo ulichukuliwa na Halmashauri Kuu ya NCCR-Mageuzi, bila kuwapa nafasi ya kuwasikiliza.
Wakili Mchau amedai kuwa, mchakato huo ulikuka sheria kwa kuwa ulikuwa na upendeleo sababu wanaodaiwa kuwa wajumbe halmashauri hiyo, walijiteua kuwa wajumbe wapya baada ya kuwaondoa wa zamani.
“Mfano mjibu maombi namba mbili (Joseph Selasini) ambaye aliteuliwa kama mdhamini mpya alikuwa ni mjumbe wa halmashauri hiyo hiyo na hapohapo akajiteua kuwa mdhamini. Hivyo, mjibu maombi wa kwanza hadi wa sita waliwafukuza waleta maombi halafu wakajiteua wenyewe,” amedai Wakili Mchau.
Katika hoja nyingine, Wakili Mchau amedai kwamba kikao kilichofanyika tarehe 21 Mei 2022, kinachodaiwa kuwa cha Halmashauri Kuu ya NCCR-Magezi na kuwaondoa wajumbe hao, kilikuwa batili kwa kuwa hakikuhudhuriwa na viongozi wa Serikali.
Wakili Mchau alidai kuwa, wajumbe hao walifukuzwa kinyume cha katiba ya NCCR-Mageuzi, kwa kuwa halmashauri hiyo haikuzingatia masharti yaliyowekwa katika katiba hiyo ikiwa mjumbe wa bodi ya wadhamini amekosa sifa za kuendelea kushika wadhifa huo.
Amedai kuwa, katiba ya NCCR-Mageuzi inaelekeza mjumbe wa bodi hiyo anapaswa kuondolewa ikiwa ana afya mbaya, atakuwa na uwezo mdogo wa kufanya kazi, ataishi nje ya nchi kwa miaka miwili mfululizo na kukiuka katiba ya chama hicho.
Lakini halmashauri hiyo kupitia maazimio yaliyotangaza kuwaondoa wajumbe hao, ilieleza sababu za uamuzi ni wahusika kushindwa kutoa taarifa juu ya uuzaji wa nyumba iliyokuwa maeneo ya Bunju B jijini Dar es Salaam, ambayo ni Mali ya NCCR-Mageuzi.
Aidha, Wakili Mchau amedai kwamba kikao hicho kinachodaiwa kuwa cha Halmashauri Kuu ya NCCR-Mageuzi, hakikuwa halali kwa kuwa hakikuwa na ajenda ya kuwaondoa wajumbe wa bodi ya wadhamini.
Naye mleta maombi wa kwanza ambaye alikuwa mjumbe wa zamani wa bodi ya wadhamini,Mohamed Tibanyendera, akijitetea mahakakani hapo amedai waliondolewa kinyume Cha sheria Kwa kuwa hawakupewa wito wa kufika katika kikao kilichowaondoa.
Tibanyendera aliiomba mahakama hiyo itamke kwamba yeye na wenzake wanne waliondolewa ujumbe wa bodi hiyo, ni halali.
Jaji Kisanya ameahirisha kesi hiyo hadi kesho tarehe 25 Januari 2023, saa 4.30 asubuhi.
Katika kesi ya msingi, wajumbe hao wanapinga mchakato uliotumika kuwaondoa madarakani viongozi wa NCCR-Mageuzi, akiwemo aliyekuwa Mwenyekiti, Francis Mbatia na wanachama wengine.
Leave a comment