WAFUASI wa Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, anayedaiwa kufukuzwa James Mbatia, wamepanga kufanya mikutano ya hadhara Januari 2023. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 7 januari 2022 na Mkuu wa Idara ya Uenezi na Mahusiano ya Umma NCCR-Mageuzi, Edward Simbeye, akizungumza na MwanaHALISI Online, kuhusu hatua ya Rais Samia Suluhu Hassan, kuondoa zuio la mikutano ya hadhara.
“Nikisema hatufanyi mikutano nitakuwa muongo, sisi tunafanya na tutawatangazia muda si mrefu. Ratiba itatolewa baada ya kukutana na kushauriana ila huenda ikawa Januari hii,” amesema Simbeye.
Alipoulizwa kwamba watafanyaje mikutano hiyo wakati wamefukuzwa ndani ya NCCR-Mageuzi, Simbeye alisema wao pamoja na mwenyekiti wao, Mbatia hawakufukuzwa na kwamba wamekwenda mahakamani kupinga hatua hiyo kwa kuwa ilikuwa kinyume cha sheria.
“Mwanachama yeyote ana haki ya kufanya mikutano ya hadhara, mimi sijafukuzwa mpaka leo na sina barua ya kufukuzwa sababu mimi ni kiongozi ili unifukuze lazima uniletee barua. Kwa upande wetu hakuna aliyepewa barua ya kufukuzwa ni matamko tu yalitolewa ambayo kimsingi hatuwezi kuyafanyia kazi na ndiyo maana tumefungua kesi kama viongozi,” amesema Simbeye.
Mtandao huu ulimuuliza Simbeye ni hatua gani watakazochukua endapo watazuiwa kufanya mikutano hiyo, alijibu akisema “hatuwezi kutabiri, subiri tuzuiwe ili tutoke tuseme.”
Mgogoro ndani ya NCCR-Mageuzi uliibuka Septemba 2022, baada ya unaoitwa mkutano mkuu wa chama hicho kumvua uenyekiti pamoja na kumfukuza Mbatia, ambapo Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, ilipiga marufuku mwanasiasa huyo na wengine wanaodaiwa kufukuzwa kujishughulisha na shughuli za chama hicho.
Hata hivyo, Mbatia na wenzake wamefungua kesi katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, kupinga uamuzi huo wakidai haukuwa halali. Kesi hiyo bado iko mahakamani na haijatolewa uamuzi.
Leave a comment