SIKU chache baada ya wafungwa watatu wa ugaidi nchini Kenya kutoroka katika gereza lenye ulinzi mkali, askari saba waliokuwa wanalinda gereza hilo la Kamiti Maximum wamesimamishwa kazi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hatua hiyo imekuja baada ya wafungwa hao hatari Musharaf Abdalla Akhulunga maarufu Zarkawi au Alex au Shukri; Mohamed Ali Abikar na Joseph Juma Odhiambo maarufu Yusuf kutoroka kwenye gereza hilo lenye ulinzi mkali baada ya kuvunja sehemu ya ukuta.
Watatu hao walitoroka usiku wa kuamkia Jumatatu tarehe 15 Novemba, 2021 na sasa tayari polisi wameanzisha msako mkali kwa wafungwa hao.
Mkurugenzi wa Idara ya Uchunguzi kuhusu Uhalifu (DCI), George Kinoti alitangaza zawadi ya Sh bilioni 1.2 kwa yeyote atakayetoa habari zitakazowasaidia kukamata wahalifu hao.
Musharaf Abdalla Akhulunga alikamatwa Septemba 30, 2012 kwa kujaribu kulipua majengo ya Bunge.
Mohamed Ali Abikar alikamatwa mwaka 2015 kwa kushiriki katika mipango ya kutekeleza shambulio la ugaidi katika Chuo Kikuu cha Garissa.
Wakati Joseph Juma Odhiambo alikamatwa mwaka 2019 katika eneo la Bulla Hawa, Somalia alipokuwa akienda kujiunga na magaidi wa Al-Shabaab.
Taarifa iliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani nchini humo, Fred Matiang’i imesema; “Tutafanya msako mkali kuwatafuta watu hawa watatu. Ni wahalifu hatari na lazima tuwapate.
“Tutachukua hatua thabiti kuhakikisha uzembe wa aina hii hautokei tena.”
Naye Kamishna Mkuu wa Magereza nchini humo, Wycliffe Ogallo alisema tayari vituo vyote vya polisi vimepewa taarifa kuhusiana na wafungwa hao.
Mkuu huyo wa taasisi za kurekebisha tabia aliwataka wananchi walio na habari kuhusiana na wafungwa hao kutoa taarifa polisi habari kupitia nambari 999112.
Kamiti Maximum ni kati ya magereza yenye ulinzi mkali zaidi nchini. Kutoroka kwa wafungwa hao kumeibua maswali kuhusu ulinzi wa magereza nchini humo.
Leave a comment