UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), mkoani Shinyanga, wameuomba Rais Samia Suluhu Hassan, apunguze kiwango cha tozo ya mitandao ya simu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga…(endelea).
Wito huo ulitolewa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Shinyanga, Baraka Shemahonge, katika kikao cha baraza hilo, kilichofanyika mkoani humo na kuhudhuriwa na Naibu Waziri wa Vijana, Kazi na Ajira, Patrobas Katambi.
Shemahonge alisema kuwa, tozo hiyo itapunguza ajira za vijana waliojiajiri katika biashara ya fedha za mtandaoni, kwa kuwa mzunguko wa miamala ya fedha itapungua, kutokana na watu kukwepa makato hayo.
‘Tunamuomba Rais Samia alitazame upya suala zima la tozo za miamala ya simu. Tunaona vijana wengi watakosa ajira, kwa sababu mzunguko wa miamala ya simu utapungua,” alisema Shemahonge.
Aidha, Shemahonge alisema, tozo hizo zitaathiri pia wananchi wa maeneo ya vijijini ambao wanategemea huduma ya fedha za mitandaoni kutokana na maeneo hayo kukosa huduma za benki.

“Lakini wazee na wananchi waliopo vijijini wataathirika, kwa sababu kule hakuna benki, wengi wanatumia simu katika kutuma na kupokea fedha, makato haya yanakwenda kuathiri moja kwa moja wananchi wenye kipato cha chini,” alisema Shemahonge.
Tozo hizo zilianza kutumika tarehe 15 Julai 2021, baada ya kupitishwa katika Bunge la Bajeti, lililoisha Juni mwaka huu.
Kwa mujibu wa tozo hiyo katika miamala ya simu, Serikali inatoza kuanzia Sh. 10 hadi 10,000 , katika muamala wa kutuma au kutoa pesa, kulingana na thamani ya muamala wa fedha husika.
Baada ya tozo hiyo kuanza kutumika, baadhi ya wananchi wameiomba Serikali ipunguze kiwango cha tozo hiyo.
SERIKALI BAADA YA KUCHOKAA KUKIMBIZANA NA MO DEWJI,SAID BAHRESSA SASA HIVI WAMEONA WAWAKAMUWE DAMU WALALAHOI MALOFA HADI WATOKE MAJI ILIMRADI PESA ZIPATIKANE ZA KUWALIPA MA BWANYEYE,MISHAHARA SPIKA, WABUNGE,MAWAZIRI,MANAIBU,RAIS,MAKAMO WA RAIS ,WAZIRI MKUU,NA WAKUU WA MIKOA NA WA WILAYA,PAMOJA NA HAO WANAO WAWEKA MADARAKANI JESHI LA POLISI.
Waliokuwa wakikamuliwa walikuwa wafanyabiashara na baada ya biashara kudorora, wananchi washangiliaji TU wa miradi mikubwa nao waichangie na waone joto ya jiwe. Hiyo ndio mantiki ya kodi hii. Saafi saana.