MIONGONI mwa sababu za January Makamba, aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kung’olewa kwenye nafasi hiyo, zimetajwa. Anaandika Regina Mkonde … (endelea).
Akizungumza kwenye hafla ya kuwaapisha George Simbachawene (Mazingira) na Hussein Bashe (Kilimo), leo tarehe 22 Julai 2019 Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais John Magufuli ameeleza kukerwa na ucheleweshwaji katika kutekeleza maagizo pamoja na fedha za wafadhili kutoonekana kulisaidia taifa kwenye mazingira.
Bila kumtaja jina (Makamba) aliyekuwa akiongoza Wizara ya Mazingira, ameeleza kumekuwepo na fedha nyingi zikitolewa na wafadhili kwa ajili ya mazingira, lakini hazionekani katika utekelezaji wake.
Rais Magufuli alimwondoa Makamba kwenye serikali anayoiongoza jana tarehe 21 Julai 2019, na kumteua Simbachawene kushika nafasi yake huku Hussein Bashe, Mbunge wa Nzega akiteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Kilimo.
Akizungumzia kauli ya Simbachawene kuhusu matumizi yasiyoridhisha ya fedha za wafadhili, Rais Magufuli amesema kuwa fedha nyingi zinatolewa lakini hazionekani matumizi yake.
“Fedha nyingi tu zinatolewa na wafadhili lakini haziwi reflected (hazionekani) kwenye miradi husika, kuna miradi mingine ilikuwa hewa kule Rufiji, ikapandwe mikoko mikoko haipo, nataka haya ukayashughulikie.
“Nakumbuka kwenye suala la mifuko ya plastiki, lilichukua muda mrefu… (kama) miaka minne, nikasaini halikutekelezwa. Makamu wa rais akazungumza wee, halikutekelezwa.
“Waziri Mkuu akaenda kulizungumza bungeni, halikutekelezwa mpaka mwishoni nilipotoa amri ya lazima ndipo likaanza kutekelezwa, usiende kufanya hivyo, wewe ukayatekeleze hayo sababu ndiyo uliyoyaapa,” amesema Rais Magufuli.
Kabla ya Rais Magufuli, Simbachawene aliseme kumekuwepo na fedha nyingi zinazoingizwa kupitia taasisi binafsi (NGO), lakini hazionekani kusaidia mazingira.
“Nafahamu kwamba nchi yetu inayo matatizo makubwa sana eneo la mazingira, ziko rasilimali fedha nyingi zinaingia kupitia sekta binafsi-NGOs, hata huduma haziendi moja kwa moja kutatua mazingira bali yanatumika katika utawala zaidi.
“Kinachokwenda kwenye mazingira ni kidogo, hasa tunavyoona hali ya uharibifu wa mazingira kwenye maeneo tunayoishi…,fedha zinazotajwa kuingia katika nchi ni nyingi lakini haziingi kwenye matatizo yaliyiopo,” alisema Simbachawene.
Leave a comment