KILELE cha Wiki ya Mwananchi cha mabingwa wa kihistoria nchini Tanzania, Yanga ya jijini Dar es Salaam, kimehitimishwa kwa majonzi baada ya kupokea kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Zanaco ya Zambia. Anaripoti Mintanga Hunda, TUDARCo…(endelea).
Mchezo huo umechezwa kuanzia saa 1:00 usiku leo Jumapili tarehe 29 Agosti 2021, katika dimba la Benjamin Mkapa mkoani Dar es Salaam.
Yanga ikicheza mchezo huo katika dimba lililokuwa limeujaza uwanja huo wenye uwezo wa kubeba mashabiki 60,000 waliokaa, wamekubali kipigo hicho.
Mashabiki walitarajia kuona ushindi kati ya timu zake tatu za vijana, wanawake na wakubwa lakini zote zimekuwa na matokeo yasiyoridhisha.
Mechi ya kwanza ilikuwa ya Vijana (U20) waliokubali kipigo cha 3-1 kutoka kwa Cambiaso na mchezo wa pili wa Yanga Princess dhidi ya Ilala Queens umemalizika kwa sare ya 1-1.
Katika mchezo wa Yanga na Zanaco, mshambuliaji wao aliyerejea Harieth Makambo aliifungia bao la kuongoza dakika ya 30 ya kipindi cha kwanza, baada ya kuwachambua mabeki wa Zanaco.
Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika Yanga iliyokuwa imevalia jezi yao mpya ya bluu iliyozinduliwa hivi karibuni, ilikuwa ikiongoza kwa 1-0.
Kipindi cha pili kilipoanza, Yanga ilifanya mabadiliko kadhaa kwa wachezaji ikiwemo jezi za juu kwa kuvaa za njano.
Mabadiliko hayo kwa Yanga hayakuwa na faida kwani Zanaco ambayo imemaliza nafasi ya pili ya Ligi ya Zambia, ikionekana kuwashambulia vilivyo Yanga.
Hadi dakika ya 77 inafika, Zanaco walikuwa tayari wamewashushia kipigo Yanga na kuufanya uwanja kuwa tulivu kwa wananchi wasiamini wanachokiona.
Furaha pekee ambayo Yanga wameipata wakati katika dimba hilo ni burudani iliyotumbuizwa na wasanii mbalimbali akiwemo Koffi Olomide wa Congo.
Leave a comment