MKUU wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Jakaya Kikwete ametaka utafiti ufanyike ili kujua kwa nini idadi ya wanaume katika kujiunga na taaluma kwenye chuo hicho imepungua, kwa kuwa katika udahili wake wa 2022 wanawake wameongezeka na kufikia asilimia 53. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Kikwete ambaye ni Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Nne, ametoa kauli hiyo leo Jumatano, tarehe 30 Novemba 2022, katika mahafali ya 52 ya duru ya tano ya UDSM.
Ni baada ya Makamu Mkuu wa UDSM anayeshughulikia Taaluma, Prof. Boniventure Rutinwa, kusema kuwa wanafunzi 313 kati ya 640 (50%), waliopata ufadhili wa masomo kutoka Ufadhili wa Rais Samia Suluhu Hassan, wamejiunga na chuo hicho.
“Tuseme katika udahili mwaka huu asilimia 53 ni wanawake, sasa sijui watoto wa kiume wamekwenda wapi siku hizi, itabidi suala hili tukae na kulifanyia utafiuti huko waliokwenda sijui ni wapi,” amesema Dk. Kikwete.
Aidha, Dk. Kikwete amepongeza kitendo cha ongezeko la wanawake kujiunga chuoni hapo tena katika masomo ya sayansi, akisema huko nyuma ushiriki wao katika taaluma ulikuwa mdogo.
Leave a comment