RIDHIWANI Kikwete, Mbunge wa Chalinze mkoani Pwani ameeleza kufurahishwa na namna serikali na wadau wa maendeleo wanavyoshiriki kulivusha Jimbo la Chalinze katika vikwazo mbalimbali ikiwempo sekta ya afya. Anaripoti Yusuph Katimba … (endelea).
Ameeleza hivyo baada ya serikali kuipatia Halmashauri ya Chalinze Sh. 1.3 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo ya Kibindu, Mkange na Lugoba kwa lengo la kusogeza huduma hiyo karibu na wananchi.
Ridhiwani ametoa pongezi hizo wakati akipokea msaada wa vifaa vya ofisi kutoka Taasisi ya Tanzania Health Promotioni Support (THPS).
“Fedha hizi zimetolewa katika kutekeleza mpango wa kujenga vituo vya afya kwenye Halmashauri ya Chalinze,” amesema mbunge huyo na kuongeza;
“Kituo cha Afya Kibindu kimepatiwa shilingi milioni 420 na kituo cha afya Mkange kimepata katika hatua za mwisho kukamilika, milioni 700 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Lugoba.”
Ridhiwani amesema kuwa, pamoja na mchango wa wadau katika juhudi za kukabiliana na afya kwa wananchi wake, serikali imetoa madaktari 47 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze.
Amesema kuwa, lengo la serikali kutoa madaktari hao ni kupunguza tatizo la watoa huduma ya afya ambapo Hospitali ya Wilaya Msoga watapatiwa madaktari 10.
Ridhwani ambaye ni mtoto wa Rais wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Kikwete amesema kuwa, msaada huo unaeleza ni kwa namna gani serikali imekuwa bega kwa bega na wananchi katika kuhakikisha hawatembei umbali mrefu kupata huduma hiyo muhimu.
Mwakilishi wa THPS, Sisty Moshi amesema, taasisi yao kupitia usaidizi wa Serikali ya Marekani imekuwa ikisaidiana na serikali kutoa huduma ya afya.
Na kwamba, kwa sasa imekuwa ikijihusisha katika utoaji wa huduma kwenye Mikoa ya Kigoma, Pwani na Zanzibar na ikijielekeza zaidi katika utoaji wa huduma ya mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI katika utoaji wa huduma na tiba.
Leave a comment