Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imesema kijana Mtanzania Clemence Felix Mtenga amefariki katika mapigano yanayoendelea kati ya majeshi ya Israel na kikundi cha wanamgambo wa Hamas waliopo Ukanda wa Gaza nchini Palestina. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Jumamosi na Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali Tanzania imesema, wizara imepokea kwa masikitiko na huzuni kubwa taarifa inayothibitisha kifo cha Clemence Felix Mtenga.
Imesema Clemence ni kijana Mtanzania ambaye ni miongoni mwa Watanzania wawili ambao pamoja na raia wa mataifa mengine walikuwa hawajulikani walipo tangu yaliyopotokea mapigano tarehe 7 Oktoba 2023, nchini Israel na katika maeneo ya Wapalestina hususan Gaza.
“Marehemu Clemence alikuwa ni miongoni mwa vijana wa Kitanzania wapatao 260 waliokwenda nchini Israel kushiriki mafunzo ya kilimo cha kisasa kwa vitendo chini ya Mpango wa Ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Israel,” imesema taarifa hiyo na kuongeza;
“Tayari Wizara imechukua hatua stahiki ikiwemo kuijulisha familia na inaendelea kuwasiliana na Serikali ya Israel kuhakikisha kwamba taratibu za kuurejesha mwili wa Marehemu nchini kwa ajili ya mazishi zinakamilika kwa wakati.
Aidha, Wizara hiyo imesema inaendelea kufuatilia taarifa za Mtanzania mwingine Joshua Mollel ambaye bado hajulikani alipo tangu yalipotokea mashambulizi hayo.
“Wizara inatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki pamoja na Watanzania kwa ujumla kwa msiba huu.
“Vilevile, Wizara inapenda kuuhakikishia umma pamoja na Diaspora wa Kitanzania ikiwemo wanafunzi waliopo masomoni nchini Israel kuwa, Serikali kupitia Ubalozi wake uliopo Tel Aviv, Israel, itaendelea kuwasiliana na Mamlaka za Israel ili kuhakikisha Watanzania wote waliopo nchini humo wanakuwa salama wakati wote,” imesema taarifa hiyo.
Tarehe 26 Oktoba mwaka huu Balozi wa Tanzania nchini Israel, Alex Kallua alinukuliwa na vyombo vya habari kwamba raia hao wawili wa Tanzania ni mateka wa Hamas.
Kwa mujibu wa Israel, wageni kutoka nchi 25 kwa jumla wanazuiliwa na Hamas.
Walichukuliwa wakati wanamgambo kutoka Hamas – ambayo Israel, Uingereza, Marekani na kundi la mataifa yenye nguvu yanaitaja kama shirika la kigaidi – walipovuka hadi Israel kutoka Gaza na kuua takriban watu 1,400.
Israel tangu wakati huo imelipiza kisasi kwa mashambulizi ya anga huko Gaza, ambayo wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas inasema yameua takriban watu 6,500.
Leave a comment