ONGEZEKO la kodi limetajwa kuchochea hali ngumu ya maisha inayolalamikiwa na wananchi wengi hapa nchini, anaandika Pendo Omary.
Casimir Mabina, Mratibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Kanda ya Pwani ameuambia mtandao wa MwanaHALISI Online kwamba mzunguko wa fedha umepotea kutokana na makali ya kodi.
“Ongezeko la kodi limeathiri mambo mengi, kwa mwaka mmoja wa serikali ya awamu ya tano makali ya kodi yameongezeka na ajira zilizokuwa zikisubiriwa na watu wengi zimepeperuka ndiyo maana mzunguko wa fedha umepotea,” amesema na kuongeza;
“Bandari yetu imekosa mizigo. Tafsiri yake ni kwamba dereva wa lori la mizigo inayoenda mikoani na nje ya nchi amekosa kazi pia mama lishe aliyekuwa akimpikia dereva chakula naye hana kibarua kwa sasa.”
Mabina amesema hakuna siri kuwa hali ya sasa ya maisha ya wananchi wengi ni ngumu na uwezo wa kujipatia mahitaji yao ya kila siku umepungua kwani sukari, unga na bidhaa nyingine muhimu zimepanda bei ilihali kipato cha wananchi hakijaongezeka.
Amesema serikali inapaswa kurekebisha mfumo wa kodi ili kuwezesha uwepo kwa mfumo wa kodi utakaokaribisha wawekezaji wa ndani na nje ya nchi na kuzalisha ajira kwa Watanzania wengi.
Leave a comment