RAIS wa Tanzania, John Magufuli ametangaza maombolezo ya Kitaifa ya siku tatu kuanzia leo Jumamosi tarehe 13 hadi 15 Juni, 2020 kufuatia kifo cha Rais wa Burundi, Pierre Nkurunziza. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Nkurunzinza alifariki Jumanne tarehe 9 Juni 2020 kwa mshtuko wa moyo.
Taarifa iliyotolewa jana Ijumaa usiku tarehe 12 Juni 2020 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa imeeleza, katika kipindi chote cha siku tatu za maombolezo ya Kitaifa, bendera zote zitapeperushwa nusu mlingoti.
Rais Magufuli ameeleza, Tanzania inatoa heshima hiyo kwa kifo cha Pierre Nkurunziza kwa kutambua alikuwa Rais wa nchi jirani ambayo imekuwa na uhusiano na ushirikiano mzuri, wa kirafiki, kihistoria na kidugu na Tanzania.
“Burundi ni mwanachama mwenzetu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Mhe. Rais Nkurunziza aliipenda Jumuiya hii.”

“Pia, aliipenda Tanzania na alishirikiana nasi kila ilipohitajika, hivyo nimeona Watanzania tuungane na ndugu zetu wa Burundi katika kuomboleza na kumkumbuka Rais Nkurunziza ambaye aliiona Tanzania kama nyumbani kwake” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli amerudia kutoa pole kwa Mama Denise Bucumi, Mjane wa Rais Nkurunziza, familia, Serikali na Wananchi wote wa Burundi kwa kuondokewa na mpendwa wao na amemuombea kwa Mwenyezi Mungu aipumzishe roho yake mahali pema peponi, Amina.
Leave a comment