WANASIASA wakongwe nchini Tanzania, Mzee Joseph Butiku na Jaji Mstaafu Joseph Warioba, wamesema watamkumba aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Magufuli kutokana na msimamo wake wa kuinyoosha nchi, hasa katika maadili ya watumishi wa umma. Anaripoti Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wametoa kauli hiyo kwa wakati tofauti kutokana na msiba wa Hayati Magufuli, aliyefariki dunia Jumatano tarehe 17 Machi 2021, kwenye Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Mama Samia, Rais Magufuli alifariki dunia kwa matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo.
Tayari Mama Samia, ameapishwa leo Ijumaa tarehe 19 Machi 2021, kuwa Rais wa Tanzania.
Mzee Butiku amesema, Hayati Magufuli atakumbukwa kwa uchapakazi wake, na kuondoa dhana ya utegemezi katika ujenzi wa nchi.
“Kimsingi kwanza atakukumbukwa kwa alichotufundisha katika muda tuliokuwa nae kwamba amani na umoja haviwezi kupatikana bila kufanyia kazi, neno ninalokumbuka kwake ni ‘Hapa Kazi Tu,’ alisema mkitaka pesa inabidi wote tufanye kazi.”

“Kulikuwa na wakati Watanzania tulisuasua tukadhani tutapata barabara, dawa zetu na madaraja kwa hela ya kuombaomba. Ametufundisha tunazo hela zetu tunazoweza kutumia kuafanya kazi hizo bila kuombaomba,” amesema Mzee Butiku.
Akimzungumzia Hayati Magufuli enzi za uhai wake, Jaji Warioba amesema, aliingia madarakani katika kipindi ambacho maadili ya nchi yalikuwa yameporomoka, na kufanikiwa kuirudisha katika mstari ulionyooka.
“Alipoingia madarakani nchi ilikuwa imeingia katika hali ambayo maadili yameporomoka sana, watu walikuwa hawana nidhamu katika maisha, watu hawakuwa waadilifu,” amesema Jaji Warioba.
Amesema, alimfahamu Hayati Magufuli kwa muda mrefu na katika Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 2015, alipewa kibarua cha kumtambulisha kwa wananchi.
Mwanasiasa huyo mkongwe amesema, katika kampeni hizo alimnadi Hayati Rais Magufuli kutokana na uzalendo wake, uadilifu na mchapakazi.

“Alipogombea urais katika uzinduzi wa kampeni za CCM ya mwaka 2015, mimi nilikuwa mmoja wapo tulioombwa kumtambulisha kwa wananchi na nilikuwa nimemfahamu na nilichosema siku ile, nilisema tunahitaji kiongozi mzalendo, muadilifu ambaye ni mchapakazi na kwa kweli hilo ilikuwa imani yangu kwa Magufuli.
“Kila kiongozi ana style (aina) yake, atapata lawama hapa na pale hata Mwalimu Julisu Nyerere alikuwa analaumiwa kwa mambo mengi tu, kwa ni kawaida.
“Haishangazi na sitegemei kwamba itafika mahali ukute kiongozi hana lawama, lazima kuwe na mawazo yanayohitilafiana, ukikuta watu wanakubaliana nchi hiyo imedumaa,” amesema Jaji Warioba.
Kuhusu uongozi mpya wa Rais Samia Suluhu Hassani, Jaji Warioba amesema anaamini kiongozi huyo atakuwa mfano wa kuigwa kwa wanawake.
“Sitegemei kama kutakuwa na matatizo yoyote tunajua, Mama Samia ataapishwa tu, atakuwa rais na atapendekeza nani msaidizi wake, atapeleka bungeni litamkubalia, naamini ataonesha kwa mfano kwamba hata wanawake wanaweza kwa uongozi, hilo tunafahamu na sisi tutamuunga mkono,” amesema Jaji Warioba..
Leave a comment