RAIS wa Tanzania, John Magufuli ametangaza siku tatu za maombolezo ya Kitaifa kuanzia leo Jumatano tarehe 17 Februari 2021, ambapo bendera zote zitapepea nusu Mlingoti, kufuatia kifo cha Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Maalim Seif (77), amekutwa na mauti leo Jumatano saa 5:26 asubuhi, katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam, alipokuwa akipatiwa matibabu.
Taarifa iliyotolewa na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, imesema, Rais Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Zanzibar, Hussein Mwinyi kufuatia kifo cha Maalim Seif.
Katika salamu hizo, Rais Magufuli amemuomba Rais Mwinyi kufikisha salamu za pole kwa familia ya marehemu, Wazanzibari wote, Wanachama wa ACT – Wazalendo, ndugu, jamaa na marafiki wote walioguswa na kifo hicho
“Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar. Natoa pole kwa Rais wa Zanzibar Mhe. Dkt. Mwinyi, Familia, Wazanzibari, wanachama wa ACT-Wazalendo na Watanzania wote. Mungu amuweke mahali pema peponi, Amina” amesema Rais Magufuli.
Awali, akitangaza taarifa za kifo hicho, Rais Mwinyi alitangaza siku saba za maombolezo kwa upande wa Zanzibar kuanzia leo Jumatano ambapo bendera zitapepea nusu mlingoni.
Leave a comment