SHEIKH Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, leo tarehe 11 Juni 2019 anapandishwa kizimbani kwenye Mahakama ya Rufani, jijini Dar es Salaam baada ya serikali kumkatia rufaa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Kiongozi huyo wa Kiislam, anapandishwa tena kizimbani kusikiliza rufaa katika Mahakama ya Rufaa baada ya serikali kutoridhishwa na uamuzi wa Mahakama Kuu kumfutia hukumu ya Mahakama ya Kisutu katika kesi ya jinai namba 245 ya 2012.
Jaji Augustine Shangwa wa Mahakama Kuu, tarehe 27 Novemba 2014 alifuta hukumu iliyotolewa na Mahakaka ya Kisutu iliyomtia hatiani Sheikh Ponda, kwenye kesi yake ya uvamizi wa kiwanja cha Markaz kilichopo Chang’ombe jijini Dar es Salaam.
Katika kesi hiyo iliyokuwa ikimkabili na wenzake 49, Mahakama ya Kisutu ilimtia hatiani Sheikh Ponda kwa kosa la kuingia kijinai katika eneo la ardhi ya Kampuni ya Agritanza Ltd, eneo la Chang’ombe Markazi, eneo ambalo lilikuwa likimilikiwa na Waislam.
Pamoja na Mahakama ya Kisutu tarehe 9 Mei 2013 chini ya Hakimu Mkazi Victoria Nongwa kumtia hatiani Sheikh Ponda, mahakama hiyo ilimwachia huru huku ikimpa sharti la kutotenda kosa lolote katika kipindi cha miezi 12 kwa mujibu wa kifungu ncha 25 (g) cha Sheria ya Kanuni za Adhabu.
Sheikh Ponda kupitia wakili wake Juma Nassoro, alikata rufaa hukumu hiyo katika Mahakama Kuu akieleza kutokubaliana nayo. Mahakama Kuu ilitengua hukumu hiyo na kumwacha Sheikh Ponda huru bila masharti yoyote.
Hata hivyo, serikali ilikata rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga hukumu ya Mahakama Kuu, leo Sheikh Ponda atasimama mahakamani hapo ili kusikiliza rufaa hiyo.
Leave a comment