OFISI ya Mwendesha Mashtaka ya Kijeshi imeomba kifungo cha miaka 30 jela dhidi ya Rais wa zamani wa Burkina Faso, Blaise Compaoré anayetuhumiwa kuwa mfadhili mkuu wa mauaji ya mtangulizi wake Thomas Sankara, aliyeuawa na wasaidizi wake 12 wakati wa mapinduzi ya mwaka 1987. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea)
Jana tarehe 8 Februari, 2022 Ofisi hiyo ya Mwendesha Mashtaka ya Kijeshi imeiomba mahakama imtambue Blaise Compaoré, ambaye hakufika mahakamani, kuwa ana hatia ya kuhatarisha usalama wa taifai, kuficha maiti na kuhusika katika mauaji.
Pia ofisi imeomba kifungo cha miaka 30 dhidi ya mkuu wa kikosi chake cha walinzi, Hyacinthe Kafando, ambaye pia hakuripoti mahakamani, na kifungo cha miaka 20 dhidi ya Gilbert Diendéré, mmoja wa viongozi wa jeshi wakati wa mapinduzi ya mwaka 1987.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe 1 Machi mwaka huu ambapo kesi hiyo itatajwa tena.
NI NANI ALIYEMUUA CHE GUEVARA WA AFRIKA?
Miaka 35 imepita tangu mauaji ya kushtua ya aliyekuwa rais wa Burkina Faso wakati huo Thomas Sankara yalipotokea, wanaume14 wanashitakiwa mahakamani, wakishutumiwa kushiriki katika mauaji ya mwanaume anayefahamika kama “Che Guevara wa Afrika”.
Mwanaafrika huyo mwenye haiba kubwa alipigwa risasi na kuuawa alipokuwa na umri wa miaka 37 katika mapinduzi ya tarehe 15 oktoba, 1987 yaliyomuweka madarakani rafiki yake wa karibu, Blaise Compaoré.
Miaka minne kabla, wawili hao walikuwa wamefanya mapinduzi yaliyomuweka madarakani Sankara kama rais.
Compaoré ni miongoni mwa watu 14 wanaoshutumiwa kwa mauaji ya Sankara, lakini kwa sasa yuko uhamishoni katika nchi jirani ya Ivory Coast, ambako alitorokea baada ya kulazimishwa kujiuzulu wakati wa maandamano makubwa ya mwaka 2014.
Alikanusha mara kwa mara kuhusika katika kifo cha Sankara na amesusia kesi.
Leave a comment