KESI ya kupinga kuvuliwa uanachama wa Chama cha Chadema, iliyofunguliwa na wabunge viti maalum 19 katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, imeahirishwa hadi Machi 2023, baada ya kiongozi wa Jopo la Mawakili wa chama hicho, Wakili Peter Kibatala, kupata dharura. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kesi hiyo imeahirishwa leo Jumanne, tarehe 6 Desemba 2022 na Mahakama hiyo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha, baada ya mawakili wa Chadema kupitia Wakili Jeremiah Mtobesya kuomba ahirisho akidai Wakili Kibatala, yuko nje ya Dar es Salaam.
Wakili Mtobesya amedai kuwa, Wakili Kibatala yuko jijini Mwanza kwa ajili ya kusimamia kesi ya mauaji.
Kufuatia ombi hilo, mawakili wa wabunge viti maalum walilikubali kisha Jaji Mkeha akaahirisha kesi hadi Machi 2023 kuanzia tarehe 6 hadi 9.
Kesi hiyo ilikuja kwa ajili ya usikilizwaji ambapo mawakili wa Chadema walitarajia kumaliza kumhoji maswali ya dodoso Mbunge Viti Maalum, Jesca Kishoa, kuhusu malalamiko yake ya kufukuzwa Chadema bila kupewa nafasi ya kusikilizwa.
Kesi hiyo itakapokuja kusikilizwa Machi 2023, Kishoa ataendelea kuulizwa maswali ya dodoso na mawakili wa Chadema. Alianza kuhojiwa tarehe 9 Novemba 2022.
Leave a comment