MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, imeifuta kesi ya kikatiba Na.21/2021, iliyofunguliwa na kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo cha Chadema, Freeman Mbowe, kupinga utaratibu uliotumika kumkamata jijini Mwanza, kumuweka kizuini na kumfungulia kesi ya ugaidi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar ea Salaam … (endelea).
Kesi hiyo iliyokuwa inasikilziwa na jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, wakiongozwa na Jaji John Mgetta, imefutwa leo Alhamisi, tarehe 23 Septemba 2021 na mahakama hiyo.
Kesi hiyo imefutwa kufuatia upande wa Jamhuri, kuweka mapingamizi manne juu ya kesi hiyo iliyofunguliwa na Mbowe dhidi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG). Ukidai ni batili kwa kuwa ina upungufu wa kisheria.
Akisoma hukumu hiyo, Jaji Mgetta amesema mahala sahihi kwa Mbowe kupeleka malalamiko yake ni Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, ambako kesi inayomkabili inasililizwa.
“Kwa kuwa Mbowe analalamika tangu akamatwe Mwanza na kufunguliwa mashtaka haki zake za msingi zilivunjwa.”
“Kesi hii haiwezi kuendelea kwa kuwa Mbowe ana kesi nyingine, hii ni njia nyingine ya kuibua malalamiko yake,” amesema Jaji Mgetta
“Mahakama hii haitakuwa na mamlaka ya kuendelea na kesi hii wakati kesi nyingine inaendelea. Maombi haya nayafuta na kila mmoja abebe gharama zake,” amesema Jaji Mgetta.
Baada ya uamuzi huo, Wakili wa Mbowe, Peter Kibatala, amesema kwa sasa anaelekeza nguvu zake katika kesi ya uhujumu uchumi iliyo na mashtama ya kula njama za kufanya vitendo vya ugaidi, inayomkabili mwenyekiti huyo wa Chadema na wenzake watatu.
Wakili Kibatala amesema, malalamiko yote ya Mbowe kwa sasa yatapelekwa katika mahakama hiyo.
“Kuna njia mbadala ya malalamiko yote kuyapeleka mahakama ya mafisadi, sasa tunaelekeza nguvu zetu kwenye kesi ya jinai na hayo yalijitokeza kwenye mahakama ya mafisadi,” amesema Kibatala.
Mbowe aliifungua kesi hiyo tarehe tarehe 30 Julai 2021, akiiomba mahakama hiyo itamke mchakato uliotumika kumkamata, kumuweka kizuizini na kumfungulia mashtaka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kisha kuhamishiwa mahakama ya uhujumu uchumi, ni batili.
Katika kesi hiyo, Mbowe alidai hakupewa haki yake ya msingi ya kuwakilishwa na mwanasheria wake wakati anahojiwa baada ya kukamatwa Mwanza, usiku wa kuamkia tarehe 21 Julai 2021.
Pia, alidai hakupata nafasi ya kupewa chaji ya mashtaka baada ya kukamatwa.
Kesho Ijumaa, Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam itaendelea kusikiliza kesi ndogo kati ndani ya kesi kubwa inayowakabili Mbowe na wenzake watatu kwa shahidi wa tatu upande wa jamhuri kuendelea kutoa ushahidi.
Leave a comment