WAKILI wa utetezi katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake, katika Mahakama ya Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Ujujumu Uchumi, Peter Kibatala, amedai mahakamani hapo kwamba, mshtakiwa wa pili, Adam Kasekwa aliwahi kuwa na matatizo ya akili. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mbali na Mbowe ambaye ni mshtakiwa wa nne na Kasekwa, washtwakiwa wengine ni , Halfani Bwire Hassan (wa kwanza) na Mohammed Abdilah Ling’wenya (wa tatu).
Wakili Kibatala alitoa madai hayo jana tarehe 15 Septemba 2021, mahakamani hapo mbele ya Jaji Mustapha Siyani, wakati anamhoji (Cross Examine), shahidi wa kwanza wa Jamhuri, ACP Ramadhan Kingai, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi na Makosa ya Jinai mkoani Arusha.
Alikuwa anamhoji ACP Kingai katika shauri dogo la kesi hiyo ya uhujumu uchumi, yenye mashtaka ya kula njama za kufanya ugaidi, inayomkabili Mbowe na wenzake, lilitokana na mapingamizi ya Mawakili wa utetezi wakiongozwa na Kibatala.
Wakipinga Kamanda huyo, asitumie maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo, Kasekwa. Kama kielelezo, kwa madai yalichukuliwa nje ya muda kisheria, pamoja na mshtakiwa kulazimishwa kuyatoa pasina hiari yake.
Wakili Kibatala alitoa madai ya kwamba mshtakiwa huyo aliwahi kuwa na matatizo ya akili, baada ya ACP Kingai ambaye kwa sasa ni Kamanda wa Jeshi la Polisi, Mkoa wa Kipolisi Kindoni, Dar es Salaam, kudai mahakamani kwamba Kasekwa alihojiwa huku akiwa hana matatizo ya kiafya.
Wakili Kibatala alidai, Kasekwa alipata matatizo hayo akiwa Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kabla ya kufukuzwa kazi kwa sababu mbalimbali.
Akimhoji shahidi huyo, Wakili Kibatala alimuuliza kama wakati anamhoji mtuhumiwa huyo, alifahamu au hakufahamu kwamba alipata tatizo la kisaikolojia.
Ambapo Kamanda Kingai alijibu, alifahamu baada ya kuambiwa na mtuhumiwa huyo.
Akiendelea kumuuliza Kamanda Kingai, Wakili Kibatala alimuuliza kama anafahamu ugonjwa huo ni wa akili, ambapo alijibu hafahamu akidai kuwa yeye sio daktari.
Aidha, Wakili Kibatala alimuuliza Kamanda Kingai kama alifuatilia taarifa za mtuhumiwa huyo kuwa na matatizo hayo, ikiwemo kumuota daktari amchunguze kabla ya kumhoji.
Ambaye alijibu akidai hakumuita.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa leo Alhamisi, tarehe 17 Septemba 2021, mahakamani hapo, ambapo Kamanda Kingai anaendelea kutoa ushahidi wake kwa kuhojiwa na upande wa Jamhuri.
Katika shauri hilo dogo, upande wa Jamhuri umepanga kuita mashahidi saba, akiwemo Kamanda Kingai, ambaye anatarajiwa kumaliza kutoa ushahidi wake leo.
Asante sana kwa kutushirikisha taarifa hii. Nimependa sana mpangilio wa taarifa hii.
Inanifanya nijione kama nilikuwepo eneo la tukio.
Rafiki yako,
Aliko Musa.
Real estate investment consultant