MAHAKAMA Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, imeahirisha kesi ya uhujumu uchumi, inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake, hadi kesho Alhamisi, tarehe 10 Februari 2022, baada Mkaguzi wa Polisi, Tumaini Swila kushindwa kuendelea kutoa ushahidi wake, akidai anaumwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Amri hiyo imetolewa leo Jumatano, tarehe 9 Februari 2022 na mahakama hiyo mbele ya Jaji Joachim Tiganga, baada ya Inspekta Swila kudai hawezi kuendelea kutoa ushahidi kwa kuwa hali yake kiafya si nzuri.
Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni waliokuwa makomando wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdillah Ling’wenya.
Jaji Tiganga alimuamuru Inspekta Swila, kesho atakapofika mahakamani hapo, awasilishe uthibitisho ya kuwa alipata matibabu hospitalini.
” Kuhusiana na aje na uthibitisho kuthibitisha mahakamani kuwa anaumwa, mahakama inaona ni busara shahidi aje na uthibitisho, usiwe na details ya ugonjwa wake na matibabu aliyopata. Itoshe kusema ametibiwa,” amesema Jaji Tiganga na kuongeza:
“Naahirisha shauri hili hadi kesho saa 3 asubuhi na shahidi nakuonya kwamba kesho urudi mahakamani na uje na uthibitisho ambao si lazima uwe na ugonjwa wako lakini uoneshe kwamba umepata matibabu.”
Jaji Tiganga alitoa amri hiyo, baada ya Inspekta Swila ambaye ni mpelelezi msaidizi wa kesi hiyo, akiwa katikati ya mahojiano yake na Kiongozi wa Jopo la Mawakili wa Utetezi, Peter Kibatala, kudai hali yake kiafya si nzuri.
Wakili Kibatala alikuwa anamuuliza maswali ya dodoso.
“Samahani mheshimiwa Jaji sijisikii vizuri kuendelea kutoa ushahidi, hali yangu kiafya si nzuri,” amedai Inspekta Swila.
Shahidi huyo 13 wa Jamhuri, alitoa madai ya kuwa hali yake kiafya si nzuri kwa mara ya pili, ambapo mara ya kwanza aliitarifu mahakama hiyo kuwa kuanzia jana jioni hali yake haikuwa nzur lakini ataendelea kutoa ushahidi.
“Mheshimiwa Jaji kuanzia jana jioni hali yangu haikuwa nzuri, lakini nitaendelea kutoa ushahidi,” amedai Inspekta Swila.
Kufuatia ombi hilo , Kiongozi wa Jopo la Mawakili wa Utetezi, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Robert Kidando, aliomba kesi hiyo iahirishwe hadi kesho.
Hata hivyo, Wakili Kibalata alipinga ombi hilo akidai “sisi tunaamini ingawa sio madaktari, ahirisho hili ni kwa sababu nyingine si kwa hali ya afya ya shahidi. Lakini tuiachie mahakama.”
Wakili Kibatala aliiomba mahakama hiyo imuamuru Inspekta Swila, alete uthibitisho kuwa amepata matibabu, akidai ana wasiwasi na madai yake kuwa hali yake kiafya sio nzuri.
“Kama tulivyo propose iahirishwe hadi saa 9 alasiri au kesho na kama walivyo-propose (pendekeza) upande wa mashtaka, shahidi aje na uthibitisho kwamba ame-attend hospitali na ametibiwa,” amedai Wakili Kibatala.
Wakili Kibatala amedai kuwa, kuna baadhi ya mashahidi waliwahi kudai wanaumwa na kushindwa kuendelea kutoa ushahidi wao lakini hawakuleta uthibitisho kutoka hospitali, unaothibitisha walipatiwa matibabu.
“Naikumbusha mahakama kwamba kuna foundation ya haya . Huyu tutakuwa tunaahirisha shahidi kwa namna hii itakuwa ni mara ya tano au nne. SP Jumanne Malangahe tuliambiwa, lakini haikuletwa ushahidi wowote. Wakati wa cross examination, Inspekta Innocent Ndowo aliomba akasema anaenda hospitali, hawakuleta uthibitisho wowote,” amedai Wakili Kibatala na kuongeza:
“Washtakiwa wana haki na morali ya kufahamu shauri lao kama mashahidi wanalipa seriouseness inayostahili.”
Wakili Kidando aliijibu hoja ya Wakili Kibatala, akidai si afya kwa afisa wa mahakama kutuhumu jambo ambalo hana uhakika nalo.
“Wenzetu wanaituhumu hiyo hali wanayosema ya shahidi, sisi tunaona kama maofisa ya mahakama kusema wenzetu nadhani hana uhakika wa anachokisema. …
Leave a comment