MAWAKILI wa utetezi, katika kesi ya ugaidi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu, wamembana shahidi wa Jamhuri, Ricardo Msemwa kuhusu vifupisho vya maneno kutofautiana na Mwongozo wa Utendajikazi wa Polisi (PGO). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Shahidi huyo amehojiwa leo Jumatatu, tarehe 22 Novemba 2021, Mahakama Kuu, Divisheni ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, jijini Dar es Salaam, wakati akitoa ushahidi wake kwenye kesi ndogo ndani ya kesi ya msingi.
Alikuwa akitoa ushahidi wake katika kesi hiyo ndogo ya kupinga maelezo ya onyo ya mshitakiwa, Mohamed Ling’wenya yasipokelewe mahakamani hapo kwa madai hakuandika alipokuwa kituo kikuu cha polisi Dar es Salaam na au kituo cha Mbweni jijini humo.
Hoja ya vifupisho hivyo, iliibuliwa na wakili John Mallya akitaka kujua
sababu za kifupisho cha Kituo kikuu cha Polisi Dar es Salaam kutofautiana na Mwongozo wa Utendajikazi wa Polisi (PGO).
Mallya: Nikuulize shahidi kwa mujibu wa hii nyaraka ya polisi hivi vifupi CD, IR vinawekwa sababu vimeandikwa mujibu wa sheria?
Shahidi: Ni vifupi kwa mujibu wa PGO.
Mallya: Kwa hiyo CD ni Central Dar es Salaam?
Shahidi: Ndio
Mallya: Nina PGO unioneshe lini uliona kituo kikuu cha polisi Dar es Salaam kifupi chake CD?
Shahidi: Hii central PC Dar es Salaam, inawezekana ikawa Polisi School inawezekana ni collage ila mimi ninavyofahamu ni Central Dar es salaam.
Mallya: PGO namba tano inazungumzia vifupisho vya vituo vya polisi Tanzania, sasa hapa kuna vifupisho vyote vya vituo, central ya miaka mingi tutafutie tuoneshe central CD?
Shahidi: Anatafuta
Mallya: Mimi nimetafuta tangu jana nikakosa
Shahidi: Mheshimiwa jaji kwa hapa sijaiona
Mallya: Angalau kwenye PGO, CD haionekanani au angalu haipo?
Shahidi: Kwa mimi sijaiona.
Mallya: Ili tuamini kimetoka central, tungeona walau jina kwa kirefu chake au kifupi kilichoandikwa kwenye PGO hatujaiona, je hiki DR ina makosa?
Shahidi: Haina makosa
Mallya: Basi PGO ina makosa?
Shahidi: Kimyaaa..
Mallya: Soma kifungu kimeandikwaje?
Shahidi: Central PC, Dar es Salaam.
Mallya: Kitu gani hakiko sahihi PGO au karatasi lako?
Shahidi: Kitabu cha central kipo sahihi kutokana na kitabu chenye taarifa za mahabusu
Mallya: Kwa hiyo PGO haiko sahihi?
Shahidi: Sijajua kipi kitapimwa lakini kitabu cha DR kiko sahihi
Katika eneo hilo, wakati wa maswali ya ufafanuzi, wakili wa serikali Pius Hilla alimtaka shahidi huyo atoe ufafanuzi kuhusu suala hilo kuhusu kifupisho CD.
Kwenye majibu yako ukawa unasema DR haina makosa na PGO haina makosa ifafanulie mahakama kule central hizi CD ni kifupisho kwa ajili gani?
Shahidi: Navyofahamu mimi ni kifupisho cha CD Dar es Salaam na kwamba hutakuta katika kituo chochote Tanzania kwa hiyo haipatikani kituo chochote kile Tanzania nzima
Kesi hiyo itaendelea tena kesho kwa shahidi wa tatu wa Jamhuri kutoa ushahidi wake.
Leave a comment