MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi imeipiga karenda kesi inayowakabili viongozi waandamizi tisa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) akiwemo Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, mpaka Septemba 27 mwaka huu. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Watuhumiwa kwenye kesi hiyo ni pamoja na Freeman Mbowe Mwenyekiti wa Chadema, Vicent Mashinji Katibu wa Chadema, Halima Mdee, Mbunge Kawe John Mnyika Mbunge wa Kibamba na Easter Bulaya Mbunge wa Bunda. Salum Mwalimu Naibu Katibu Zanzibar.
Wengine ni Mchungaji Peter Msigwa Mbunge wa Iringa Mjini, Easter Matiko Tarime Mjini na John Heche Mbunge wa Tarime Vijijini.
Usikilizwaji wa kesi hiyo ulipangwa uanze leo Jumatatu Agosti 27, imeahirishwa baada ya mshtakiwa nambari tano, Ester Matiko kukosekana mahakamani.
Mdhamini wa Matiko ambae ni Diwani wa Gongo la Mboto, Dorcas Lukiko ameieleza Mahakama kuwa Matiko anaumwa na ameshauriwa na daktari wake apumzike.
Sambamba na kukosekana kwa Matiko, mshtakiwa namba mbili wa kesi hiyo, Peter Msigwa alimuomba Hakimu Mashauri ampatie muda wa wiki tatu ili atafute Wakili baada ya Wakili wake wa awali, Jeremia Mtobesya kujitoa kwenye kesi hiyo akimlaumu Hakimu Mashauri kukiuka baadhi ya taratibu za uendeshaji wa kesi.
Akiahirisha kesi, Mashauri aliwataka washtakiwa wote wafike bila kukosa siku iliyopangwa ya kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo.
Leave a comment