KITABU cha kumbukumbu za mahabusu (DR), cha Kituo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam, kimeendelea kuibua mkanganyiko katika kesi ya uhujumu uchumi, inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake kwenye Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mkanganyiko huo umeibuka leo Jumatatu, tarehe 22 Novemba 2021 mahakamani hapo mbele ya Jaji Joachim Tiganga, wakati shahidi wa pili wa jamhuri, Askari Mpelelezi, DC Ricardo Msemwa, akihojiwa na mawakili wa utetezi kuhusu kitabu hicho.
Ni baada ya kitabu hicho cha mahabusu chenye taarifa zinazodai washtakiwa wenzake Mbowe, Adam Kasekwa na Mohammed Ling’wenya, walikuwa kituoni hapo tarehe 7 Agosti 2020, kupokelewa kama kielelezo cha ushahidi wa jamhuri kwenye kesi ndogo ya kupinga maelezo ya onyo ya Ling’wenya yasipokelewe mahakamani hapo.
Mkanganyiko wa kwanza uliibuka baada ya Wakili Peter Kibatala, kumuuliza mwaka ambao kitabu hicho kilijazwa taarifa za washtakiwa hao.
Mahojiano yao ilikuwa kama ifuatavyo;
Wakili Kibatala: Hiki kielelezo kilianza kujazawa tarehe ngapi?
Shahidi: Sikumbuki
Wakili Kibatala: Naomba usome (DR), kilianza kujazwa tarehe ngapi?
Shahidi: Tarehe 24 Julai 2020
Wakili Kibatala: Entry(ingizo) ya Lin’gwenya inaanza au mwanzo au iko mbele?
Shahidi: Iko mbele
Wakili Kibatala: Hii imeacha kutumika tarehe ngapi?
Shahidi: Imeacha kutumika tarehe 12 Agosti 2020
Wakili Kibatala: Mwambie Jaji entry (ingizo) namba 310 inaonekana hiyo 2021 ni nini?
Shahidi: Hii sijui inahusiana na nini
Wakili Kibatala: Fungua Entry namba 208 umeona tarehe ngapi? Tarehe 4 Agosti mwaka gani?
Shahidi: Haisomeki
Wakili Kibatala: Hii 2021?
Shahidi: Haisomeki
Wakili Kibatala: Mwaka gani (anamuonesha DR)?
Shahidi: Hii haisomeki
Wakili Kibatala: Mimi najua ni 2021 wewe unajua mwaka gani?
Shahidi: Haisomeki
Wakili Kibatala: Fungua entry 114, hii Julai mwaka gani?
Shahidi: Mwisho wameandika 21
Wakili Kibatala: Mwaka gani iliacha kutumika?
Shahidi: tarehe 12 Agosti 2020
Wakili Kibatala: Nenda entry namba 113, tarehe 30 Julai mwaka gani?
Shahidi: Hii haisomeki
Wakili Kibatala: Hii 21 ni nini?
Shahidi: Haioneshi mwaka
Wakili Kibatala: Fungua entry 156 tarehe 2 Agosti mwaka gani? Mwisho ina maanisha mwaka gani?
Shahidi: Inamaanisha mwaka 2021
Wakili Kibatala: Hiki kielelezo kinapima ukweli na uongo wake unafahamu?
Shahidi: Nafahamu kama kinapimwa
Wakili Kibatala alimhoji Askari Msemwa kuhusu sababu za kuwatoa wa tuhumiwa hao zilizodaiwa kuandikwa katika kitabu hicho kama ifuatavyo;
Wakili Kibatala: Nilisikia mkiulizana na Wakili John Mallya sababu za kumtoa Ling’wenya ilikuwa nini?
Shahidi: Ni nje kwa upelelezi
Wakili Kibatala: Na unasema nje kwa upelelezi inajumuisha nini?
Shahidi: inajumuisha vitu vingi ikiwemo mchakato mzima wa kuanzia kesi, hadi kuifikisha mahakani.
Wakili Kibatala: Elezea wapi ulifafanua kwamba hapa alitolewa nje kwa upelelezi lakini hapa ilikuwa naamanisha nje kwa upelelezi inajumuisha kuchukua maelezo ulimwambia?
Shahidi: Mahojiano ni sehemu ya upelelezi nilitaja
Wakili Kibatala: Kutolewa nje kwa upelelezi na kutolewa nje kwa mahojiano ni sawa?
Shahidi: Sawa
Wakili Kibatala: Kwa kusoma nje kwa mahojiano na upelelezi zinafanana?
Shahidi: Hazifanani lakini ni maana moja
Hata hivyo, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Pius Hilla, alimtaka atoe ufafanuzi kuhusu utofauti huo kama ifuatavyo;
Wakili Hilla: uliulizwa swali kuhusiana na zile sababu za watu kutolewa nje mahabusu, ukasema kwa mahojiano na upelezi, ifafanulie mahakama ulikuwa na maana gani?
Shahidi: Kutolewa nje kwa mahojiano nina maana mtuhumiwa anatolewa specific kwa kuhojiwa.
Wakili Hilla: Sababu ya watu kutolewa kuna mahala uliulizwa kwa kusoma maneno tofauti, ukajibu ulimaanisha nini?
Shahidi: Nilimaanisha kwa kusoma neno mahojiano na upelelezi ni tofauti lakini mahojiano inaingia katika upelezi lakini mahojiano ni sehemu ya upelelezi.
Kada wa Chadema adai alimkuta Kituo cha Polisi Oysterbay badala ya Kituo Kikuu cha polisi Dar es Salaam.
Wakili Kibatala alimuuliza Msemwa kama anamkumbuka mwanachama wa Chadema aliyekuwa Kituo cha Polisi cha Oysterbay.
Wakili Kibatala: Kuna mtu anaitwa Lembrus Mchome unamfahamu huyu mwanachama wa Chadema, alikamatwa kwa tuhuma za kupiga picha gari ya kiongozi wa usalama alikuwa kizuizini Oysterbay unamkumbuka?
Shahidi: Simkumbuki
Wakili Kibatala: Yeye anasema Mei 2020 wewe ulikuwa Oysterbay na wewe binafsi ulimpokea ukiwa CRO duty (Afisa wa Chumba cha Mashtaka) Oysterbay 2020 wewe unasemaje?
Shahidi: Sikumbuki na pia sikuwepo Oysterbay kwa wakati huo
Wakili Kibatala: Anaweza kuwa na sababu gani za kusema uongo kuhusu wewe?
Shahidi: Sijajua sababu zake ni zipi
Wakili Kibatala: Una ugomvi naye?
Shahidi: Wala simfahamu simjui na sijui sababu ya yeye kusema uongo au kusema ukweli.
Wakili Kibatala: Tukimleta sisi kama shahidi wakati Ling’wenya anajitetea utasemaje?
Shahidi: Atasikilizwa na jaji
Ahojiwa kuhusu diary
Wakili Kibatala: Unafahamu diary uliyokutwa nayo kwenye kizimba kurasa mahsusi zinazohusiana na maeneo tuliyoangiza mahakamani unafahamu?
Shahidi: Sifahamu
Wakili Kibatala: Wakati mahakama inafanya maamuzi hukusikia wakati tunafanya maombi diary ichukuliwe na zile kurasa tunazotaka zichukuliwe ulikuwa kwenye kizimba?
Shahidi: Sikuwa kwenye kizimba
Wakili Kibatala: Ulikuwa uko wapi?
Shahidi: Mahakamani
Wakili Kibatala: Wapi tuoneshe?
Shahidi: Sikumbuki mheshimiwa jaji nilikuwa wapi, kama sio chumba cha nanii kule nilikuwa ndani
Wakili Kibatala: Angalau unafahamu kwamba diary yako ulikuwa nayo kuna kurasa fulani zinahusu kufanya ushahidi wako pamoja na kuomba iingie kwenye rekodi ya mahakama unafahamu?
Shahidi: Vitu vinavyohusiana kwenye shauri hii viko kwenye diary yangu?
Wakili Kibatala: Ndio vipo
Wakili Kibatala: Mwambie jaji kabla hujakabidhiwa kwetu kwa ajili ya cross examinatiom uliongozwa na jamhuri kufafanua chochote kuhusiana na kidhibiti namba moja (diary) ambapo ndani yake kuna vitu vinahusiana na ushahidi wako?
Shahidi: Hillo sijafafanua.
Leave a comment