MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam nchini Tanzania, imeipa siku saba Serikali kujibu kiapo kinzani kwenye kesi Na. 2 ya mwaka 2020 iliyofunguliwa na wadhamini wa Tundu Lissu, Makamo Mwenyekiti wa Chadema Bara juu ya kutaka kujitoa kwenye udhamini wa mwanasiasa huyo. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Wadhamini hao ni Lobart Katula, Meneja wa Kampuni ya uchapishaji Magezeti ya Hali Halisi Publishers na Ibrahim Ahmed, Mfanyakazi wa kampuni hiyo.
Lissu ambaye kwa sasa ni mtia nia kwenye nafasi ya Urais ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), pia Mwanasheria Mkuu wa Chama hicho anakabiliwa na kesi ya uchochezi mahakamani hapo.
Lissu ambaye hayupo nchini anashitakiwa kwenye Mahakama hiyo kwa kesi ya uchochezi namba 208 ya mwaka 2016 pamoja na Simon Mkina Mhariri Mkuu wa Gazeti la Mawio, Jabir Idrissa Mwandishi Mwandamizi wa gazeti hilo na Ismail Mahboob Meneja wa Kampuni ya uchapishaji ya Flint.
Washtakiwa hao kwa pamoja wanashtakiwa kwa makosa ya kufanya uchochezi kupitia gazeti la Mawio kwa kuchapisha habari yenye kichwa ‘Machafuko yaja Z’bar.’
Lissu ameshindwa kuhudhuria kesi hiyo tangu aliposhambuliwa kwa risasi na watu wasiojulika eneo la area ‘D’ Dodoma siku ya tarehe 7 Septemba 2017.
Wadhamini wa Lissu baada ya kuona hawana uwezo wa kumpeleka mahakamani Lissu au taarifa za matibabu yake wakati shauri hilo lilipokuwa likitajwa mahakamani hapo waliamua kufungua maombi hayo.
Leo tarehe 17 Juni 2020, Wakili wa Serikali, Wankyo Simon mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba ameiomba mahakama hiyo iwaongezee muda kwa ajili ya kuwasilisha kiapo kinzani.
Wakati huo huo, upande unaomwakilisha Lissu haukuwepo mahakamani hapo.
Hakimu Simba ameupa siku saba upande wa Jamhuri kwa ajili ya kuwasilisha kiapo hicho na kuahilisha shauri hilo mpaka tarehe 14 Julai mwaka 2020.
Leave a comment