RAIS wa Kenya, Uhuru Kenyatta ametangaza kufunguliwa kwa shule na vyuo nchini humo Septemba 1 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Kenyatta amesema hayo leo Jumamosi tarehe 6 Juni, 2020, wakati akihutubia Taifa hilo akitoa mwelekeo wa jinsi ya kukabili maambukizi ya ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19).
Amesema, maambukizo yamefikia 2,600 baada ya wagonjwa wapya 126 kupimwa corona ndani ya saa 24 na vifo vikifikia 83. Waliopona ni 643 na waliopimwa ugonjwa huo wakifikia 90,875.
Rais Kenyatta amesema, shule na vyuo zitaendelea kufungwa kutokana na hali ya maambukizi kuwa juu huku akiagiza wizara ya elimu kutoa kalenda mpya ya masomo katikati ya Agosti.
Amesema, amezungumza na wazazi, walimu na wataalamu wa afya ambao kwa pamoja wamekubaliana kutokufungua shule kwani kufanya hivyo ni hatari na hata zitakapofunguliwa, zitafunguliwa hatua kwa hatua.
“Mimi mwenyewe nilikuwa na nia ya kufungua… lakini ni mtu mjinga ambaye asikilizi kutoka kwa wataalamu wetu. Wametuambia kufungua ni makosa na kuhatarisha maisha ya Wakenya,” amesema Rais Kenyatta.
Katika hotuba yake, Rais Kenyatta amesema, zuio la usafiri wa anga litaendelea hadi hapo hali itakapokuwa imetengamaa kwa maambukizi kupungua huku akiagiza wizara ya uchukuzi kukutana na wadau wa usafiri ndani ya siku saba ili kutoa mwongozo wa usafiri huo kwa ndege za ndani.
Pia, zuio la watu kutokutoka ndani katika maeneo ya Nairobi, Mombasa, Kilifi na Kwale limeongezwa kwa siku 30 kuanzia saa 3 usiku hadi 10 alfajili. Awali, zuio la kutokutoka ndani lilikuwa likianza kuanzia saa 1 jioni hadi 12 asubuhi.
Rais Kenyatta ameendelea kupiga marufuku ya mikusanyiko kama ya kisiasa, kijamii au baa kwa siku 30.
Leave a comment