Saturday , 25 March 2023
Home Gazeti Habari za Siasa Keissy: Viongozi serikalini, CCM wamenihujumu
Habari za SiasaTangulizi

Keissy: Viongozi serikalini, CCM wamenihujumu

Spread the love

ALLY Mohamed Keissy, aliyekuwa mbunge wa Nkasi Kaskazini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania amesema, kilichomfanya akashindwa kutetea nafasi hiyo ni hujuma zilizofanywa dhidi yake na viongozi wa Serikali na CCM. Anaripoti Hamisi Mguta…(endelea).

Katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano ya tarehe 28 Oktoba 2020, Keissy alishindwa ubunge na Aida Khenani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Aida ambaye ni mbunge pekee wa Chadema aliyeibuka mshindi kwenye uchaguzi huo, alimshinda Keissy aliyeongoza jimbo hilo kwa miaka kumi mfululizo kwa kura 21,226 huku Keissy akipata kura 19,972.

Leo Jumanne tarehe 3 Novemba 2020, MwanaHALISI Online limezungumza na Keissy kutaka kujua hali ya uchaguzi ulivyokuwa na matokeo yake ambapo ameanza kwa kusema “wananchi wamenikataa wenyewe. Wananchi wamenichoka.”

Keissy amesema, wananchi wa Nkasi Kaskazini watamkumbuka jinsi alivyopambana kuwatumikia katika kipindi cha miaka kumi “kaka nikwambie, mimi nimepambana lakini ukweli wangu ndiyo umeniangusha. Viongozi mafisafi ndiyo wamenifanyia fitina.”

MwanaHALISI Online lilipotaka kujua hasa hao viongozi ni kina nani, Keissy amesema wako ndani ya CCM na wengine Serikali katika wizara ya maji.

Amesema, katika kipindi chote, amekuwa akipambana na wakandarasi wanaotekeleza miradi ya maji jimboni humo ambao wamekuwa hawampendi na wameshirikiana kuhakikisha harejei tena bungeni kwani angeendelea kuwabana.

Keissy amesema, katika mapambano hayo, alifanikiwa kuokoa fedha zaidi ya Sh.4.5 bilioni katika miradi ya maji inayotekelezwa jimboni humo “na kama utakumbuka, nimekuwa nasema sana bungeni juu ya ufisadi huu mkubwa kabisa. Mimi mwenyewe walitaka kunihonga lakini walishindwa.”

Mbunge huyo wa zamani amesema katika uchaguzi huu “walipambana kuhakikisha sirudi bungeni, viongozi wengine wako ndani ya chama na wengine wizarani, unajua kupambana na ufisadi ni kama kupambana na madawa ya kulevya. Yaani mimi maji zaidi ndiyo yamenimaliza.”

Akijibu swali la MwanaHALISI Online lililotaka kujua, alipojua kuna mafisadi wanapambana asishinde, alikishirikisha chama ili kiweze kumsaidia, Keissy amesema “chama huku ndiyo kimenimaliza, kama mwenyekiti wa CCM mkoa ni makandarasi sasa utawezaje kupona.”

Keissy amesema, Namanyere makao makuu ya wilaya “tunashida sana ya maji, hali ni mbaya na vijijini. Sasa hela zinakuja, badala ya kutatua changamoto wao wanajiongezea, mfano mradi wa Sh.3 bilioni wao wanaandika Sh.6 bilioni, mimi nikijua napiga kelele, hiyo ndiyo imenimaliza na mkandarasi mpaka leo yuko ndani.

“Nimeambiwa wakandarasi wamefanya sherehe kubwa sana baada ya haya matokeo,” amesema Keissy huku tatizo la maji jimboni humo ni kubwa ambapo viongozi wa Serikali na CCM ngazi ya Taifa wanaijua akiwaomba walifanyia kazi.

MwanaHALISI Online lilipotaka kujua hatima yake ya kisiasa baada ya hicho kilichotokea amesema, “nimeamua kuacha siasa, nibaki mwanachama wa kawaida kabisa wa CCM.”

Kuhusu hoja yale aliyoitoa Bunge lililopita ya kutaka Rais John Pombe Magufuli kuongezewa muda hata baada ya kumaliza miaka kumi yake ya uongozi amesema, ameachana nayo kwani hata bungeni hatukuwemo lakini “Rais mwenyewe amekaa hiyo hoja na hataki kuongeza muda.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Rais Samia aagiza iundwe kamati ya pamoja ya Mawaziri mradi wa BBT

Spread the love  RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewaagiza mawaziri kuunda kamati...

Habari za Siasa

Rais Samia apangua makatibu tawala mikoa, ateua Kamishna DCEA

Spread the loveALIYEKUWA Kamishna wa Mamlaka ya Kudhibiti Dawa za Kulevya, Gerald...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

M/kiti bodi ya wadhamini Chadema afariki dunia

Spread the loveMWENYEKITI wa Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Demokrasia na...

Habari za Siasa

Zitto: Nikifa Ado atavaa viatu vyangu

Spread the love  KIONGOZI Mkuu wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe...

error: Content is protected !!