KATIBU Tawala wa Mkoa wa Geita, Profesa Godius Kahyarara amewahamasisha wachimbaji wadogo wa madini mkoani humo kujiunga na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kwa ajili ya kujiwekea akiba ya sasa na ya baadae. Anaripoti Paul Kayanda, Geita … (endelea).
Kahyarara ameyasema haya leo tarehe 5 Oktoba, 2022 katika Maonyesho ya tano ya Kitaifa ya Teknolojia ya Madini mkoani humo alipozungumza na wajasiriamali pamoja taasisi za kifedha kupitia siku maalumu ya NSSF.
Siku hiyo maalum ililenga kutoa elimu kwa wajasiriamali hao na wachimbaji wa madini.
Amesema ni vizuri makundi ya wachimbaji wadogo pamoja na wananchi kwa ujumla kuwa na utaratibu wa kuhakikisha kuwa wanajiunga katika mifuko hiyo ya hifadhi ya jamii jambo ambalo litawapa faida ya kuweka akiba kwa maisha ya baadae.
“Mkoa tumeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha tunawajengea uwezo katika shughuli zenu mnazozifanya na kubwa ni kujiunga na mifuko ya hifadhi hususani Nssf kwa ajili ya akiba ya uzeeni,” amesema Professa Kahyarara
Kwa upade wake Meneja Uhusiano Elimu kwa Umma (NSSF), Lulu Menegele amesema lengo la siku hiyo ni kuongeza uelewa kwa wanachama na wachimbaji wadogo wa madinini kujiunga na Mfuko wa hifadhi ya Taifa ya Jamii Nssf.
“Tumewafikia wananchi wa mkoa wa Geita ambapo asilimia kubwa ya wachimbaji ni sehemu kubwa ya wanachama wa mfuko wa hifadhi ya Jamii. Tumewaeleza kuhusu huduma tunazozitoa kwa njia ya mbalimbali ikiwamo njia ya simu ya kiganjani na hata simu ndogo unaweza kutumia kujiunga na Nssf,” amesema Lulu.
Pia ametoa rai kwa wananchi wa mkoa wa Geita kujiunga na mfuko huyo na huduma hizo zinapatikana kwenye ofisi zote na mfuko zilizopo nchi nzima.
Naye Meneja wa NSSF mkoa wa Geita, Winniel Lusingu amesema Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Nssf hususani mkoa wa Geita unaendelea kuwahimiza wananchi kutambua umuhimu wa kujiunga na mfuko huo kwa kuwa unafaida kubwa katika maisha.
Ameongeza kupitia maonyesho ya madini wanaendelea kuandikisha wanachama wapya kwa gharama ya shilingi 20,000 huku wakizingatia kauli mbiu ya ”huduma bora kipaumbele chetu”
“Mfuko wa Hifadhi wa Jamii NSSF Mkoa wa Geita tunaandikisha wanachama pia tunawahamasisha tunapinga rushwa kwa nguvu zote.
“Katika hili nawaomba wanachama wetu kufika kwenye banda letu lililopo hapa kwenye viwanja vya maonyesho na ofisi zetu zilizopo hapa Geita ili kupata huduma zetu,” amesema Lussingu.
Wakati Meneja wa Sekta isiyo rasmi NSSF Makao Makuu, Rehema Chuma amesema mfuko huo unafikia makundi mbalimbali ya wajasiriamali ikiwemo kundi kubwa la wachimbaji wadogo la madini ya dhahabu kuwapa elimu na kuwahamasisha kujiunga na mfuko huo.
“Mfuko huu unatoa huduma nyingine ambayo utanufaika nayo ikiwa mafao ya walemavu, wajawazito na wenye matatizo mbalimbali.
“Wananufaika na mafao haya hivyo nawaasa kuchangamkia fursa hii muhimu na pia kuwekeza Nssf kwa ajili ya malengo yenu ya baadae kwani masikini wa leo ni utajiri kesho,” amesema Rehema.
Leave a comment