JUMUIYA ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imewataka wananchi wasimpelekeshe Rais Samia Suluhu Hassan, hasa wale wanaotaka mchakato wa katiba mpya ufufuliwe. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Wito huo umetolewa jana Jumanne tarehe 6 Aprili 2021, na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM, Dk. Edmund Mndolwa, akizungumza na wanahabari jijini Dodoma.
“Tunajua baadhi Watanzania wanataka katiba mpya, lakini Mama Samia kwa sasa ndiye Rais ambaye anaweza kujua nini akifanye kwa faida ya taifa,” alisema Dk. Mndolwa.
Dk. Mndolwa alisema, Rais Samia, aliyekuwa Makamu wa Rais, amefanya kazi Ikulu kwa zaidi ya miaka mitano akiwa na Hayati Rais John Magufuli, hivyo anajua kuiongoza nchi.
“Tusimpelekesha Rais wetu, yeye ni kiongozi amekuwa Ikulu na marehemu muda wa miaka sita, atakuwa anajua kila jambo. Hivyo tusiwe watu wa kumpangia nini afanye,”alisema Mndolwa.
Mama Samia aliapishwa kuwa Rais wa Tanzania tarehe 19 Machi 2021, akichukua mikoba ya Dk. Magufuli, aliyefariki dunia akiwa madarakani, tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Hadi umauti unamkuta, Dk. Magufuli aliiongoza Tanzania kwa miaka mitano na miezi minne mfululizo kuanzia tarehe 5 Novemba 2015 hadi 17 Machi 2021, akisaidiana na Mama Samia.
Dk. Mndolwa alisema jumuiya hiyo inampongeza Rais Samia kwa kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania, na kwamba itampa ushirikiano wa hali na mali katika uongozi wake.
Mbali na kuahidi kumpa ushirikiano, Dk. Mndolwa alisema jumuiya hiyo itahakikisha inampigania Rais Samia, ili awe Mwenyekiti wa CCM Taifa.
Baada ya Rais Samia kuingia madarakani, kumekuwa na kauli kutoka makundi mbalimbali wakimwomba auendeleze mchakato wa katiba mpya hasa ikizingatiwa yeye alikuwa miongoni mwa waliosimamia kupatikana kwa Katiba inayopendekezwa
Hivi karibuni, Rais Samia alizungumzia mchakato huo baada ya kuwa amejikuta akitaja jina la Bunge la Katiba badala ya Bunge la Bajeti kwenye hafla zilizofanyika Ikulu ya Chamwino, mkoani Dodoma.
Kutokana na hali hiyo, Rais Samia alisema “hivi nina maradhi gani na katiba, nafikiri wamenisukuma sukuma sana kuhusu katiba katiba lakini wasahau kidogo.”
Leave a comment