HATUA ya Rais Samia Suluhu Hassan, kuagiza wanamuziki waanze kulipwa mirabaha kutokana na nyimbo zao kupigwa kwenye redio, imemkosha msanii wa muziki wa HipHop na mwanaharakati kwenye mitandao ya kijamii, Webiro Wakazi Wassira ‘Wakazi.’ Anaripoti Matilda Peter, Dar es Saalam …(endelea).
Msanii huo alitoa kauli hiyo alipozungumza na MwanaHalisi Online mwishoni mwa wiki kwenye mahojiano maalumu kuhusu siku 100 za uongozi wa Rais Samia baada ya kuapishwa kuongoza taifa kutokana na kifo cha mtangulizi wake Hayati John Magufuli.
“Kilikuwa kilio cha muda mrefu kwa wasanii kupata haki zao, unaweza kukuta msanii ana kazi nyingi za sanaa yake, lakin kipato chake hakiendani na ukubwa wa kazi yake
“Huu ni wakati sahihi kwa wasanii kuanza kula matunda ya jasho lao, tusisubiri hadi mambo yanyooke kwani hatutafika. Tunapaswa kuanzia hapo hapo kuliko kuishi bila mirabaha, kwani huko ni kuua Sanaa,” amesema Wakazi.
Akizungumzia miundombinu ya utekelezwaji wa mirabaha kwa wasanii, ameiomba serikali kutengezea utaratibu rafiki ambao utarahisisha kazi ya kukusanya mirabaha hiyo.
Ameshauri kuhusishwa wasanii wenyewe ili kusudi waweze kushauriana namna bora za upatikanaji wa haki zao kwa kuwa, ndio walengwa zaidi na itaepusha migogoro ya mirabaha kama ilivyo Kenya.
Msanii huo amewatoa hofu wasanii chipukizi kwamba, mirabaha haiusiani na kuua vipaji vipya, zaidi itaongeza thamani ya kazi ya msanii huyo na kupata maslahi mazuri ya kazi yake.
“Tumeona nchi mbambali duniani mirabaha ikiwasaidia sana wasanii wake, hakuna historia yoyote duniani ya mirabaha kuua vipaji vipya vya wasanii,” amesema.
Leave a comment