KAMPUNI ya Mawakili ya IMMMA ya jijini Dar es Salaam, imevamiwa na watu wasiojukana na kulipuliwa kwa mabomu usiku wa kuamkia leo, anaandika Faki Sosi.
Jengo hilo lililopo eneo la Upnaga jijini Dar es Salaam lilikumbwa na mkasa huo usiku wa kuamkia leo, ambapo mabomu hayo yalibomoa madirisha, vioo kupasuliwa, mageti kuvunjwa pamoja ukuta kutobolewa.
Mmoja wa Wakurugenzi wa kampuni hiyo, Sadock Magai akizungumza na waandishi wa habari, alikiri kutokea uvamizi huo, lakini akasema hakuna mali iliyoibiwa ndani.
Magai anasema kuwa hawajajua kama kuna nyaraka zimepotea lakini kwa haraka walioangalia hakuna kitu kilichochukuliwa.
https://www.youtube.com/watch?v=veciCsG4CRg
Imeelezwa kuwa hiyo ni kampuni anayofanyia kazi Wakili maarufu nchini Fatuma Karume ambaye ni mtoto wa Rais mstaafu wa Zanzibar.
Kampuni hiyo inamilikiwa na Mawakili maarufu hapa nchini na mpaka sasa haijajulikana lengo la uvamizi huo ilikuwa ni kutaka kuiba vitu ama kudhuru wafanyakazi wake.
Jengo hilo limezingirwa na makachero wa Jeshi la Polisi ambao wameanza kufanya uchunguzi wao kuanzia mapema leo asubuhi.
Leave a comment