JESHI la Polisi, Mkoa wa Dodoma leo 22 Julai 2019 limefanikiwa kukamata kamera 12 ambazo ni mali ya Mamlaka ya Vitamburisho vya Taifa (NIDA). Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kamera hizo, ziliibiwa na ofisa usajili wa NIDA na kuziuza kwa vijana ambao ni wapiga picha.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema, jeshi hilo limekamata vifaa hivyo pamoja na mtuhumiwa.
Muroto alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Ezekiel Subugo (24), ambaye ni msajili wa NIDA anayetuhumiwa kutumia vibaya nafasi yake.
“Mbinu aliyotumia ni kutumia nafasi yake kuiba ofisini na kuuzia watu mitaani, uhalifu huu ni mbaya hasa unapohusisha mtumishi wa umma. Mtuhumiwa atafikishwa mahakamani,” amesema Kamanda Muroto.
Katika hatua nyingine, Mussa Pungu maarufu kwa jina la Mussa Nyela amekamatwa na kete 132 za dawa za kulevya aina ya heroini.
Amesema, mtuhumiwa Nyela kwa muda mrefu ameharibu vijana wengi kwa dawa za kulevya katika mtaa wa Hazina, jijini Dodoma. Mtuhumiwa na wenzake wanne watafikishwa mahakamani.
Pia jeshi hilo limemkamata Rajabu Kambi (32), mkazi wa Area “A” kwa kufanya udanganyifu, akijifanya askari polisi na kutishia watu kwa silaha bandia.
Kamanda Muroto amesema, mtuhumiwa alikutwa na sare ya polisi ‘janglegreen’, bastola bandia na picha akiwa kwenye na sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Leave a comment