JOB Ndugai, mgombea Uspika wa Bunge la 12 la Tanzania amesema, ofisi ya Bunge itatoka haki sawa kwa wabunge wote ikiwemo wa upinzani ambao hawatokuwa na Kambi Rasmi ya upinzani bungeni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea)
Ndugai amesema hayo leo Jumanne tarehe 10 Novemba 2020 wakati akijinadi kwa wabunge ili wamchague kuwa Spika wa Bunge la 12. Ndugai anatetea nafasi hiyo kwani alikuwa Spika wa Bunge lililopita la 11.
Kikao hicho cha kwanza cha mkutano wa kwanza wa Bunge la 12 cha uchaguzi wa Spika, kimeongozwa na Mbunge Mteule wa Ismani (CCM), Willium Lukuvi.
Akijinadi kwa wabunge wateule, Ndugai amewashukuru wote kwa kuchaguliwa na wananchi ili kuwa wabunge.
“Nimesimama mbele yenu kuwaomba kura ili nipate imani yenu kuwa Spika wa Bunge la 12.”
“Mkinipa nafasi hii, nitasimamia sana Katiba ya Tanzania, kanuni na taratibu mbalimbali. Ninachowaahidi, nitawatendea haki na nitalifanya Bunge la 12 kuwa la mfano ambalo halijawahi kutokea tangu Uhuru,” amesema Ndugai.

Ndugai amesema “mimi nafahamu matatizo ya wabunge, madhila ya wabunge na mambo yale. Wale wa upinzani tutawalinda kabisa bila kubaguliwa.”
Baada ya kumaliza kujinadi, Lukuvi aliuliza mwenye swali ambapo, mbunge mteule wa Nkasi Kaskazini (Chadema), Aida Khenani akauliza “mgombea, najua nafasi unayoiomba ni nafasi uliyokuwa nayo kipindi kilichopita na mwanadamu yeyote ana mapungufu.”
“Tunaomba utuambie wabunge tunaotarajia kukupa imani kwamba ulikuwa na mapungufu,” ambayo hayatojitokeza tena.
akijibu swali hilo, Ndugai ameanza kwa kumpongeza Aida kwa kumshinda, Ally Keissy “kwa sababu amemshinda rafiki yangu Ally Keissy na alikuwa anasema watatutana jimboni, kweli wamekutana.”
Ndugai amesema, ikiwa ataibuka mshindi, atasimamia usawa kwa wabunge wote na kwa kuwa “upande wa upinzani, hatutakuwa na Kambi Rasmi ya Upinzani kwa kuwa hawatatimiza asilimia 12, uongozi wa spika, ofisi ya Bunge tutawatendea haki kabisa.”
Hata hivyo, ingawa Ndugai ametumia neno la Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, mabadiliko yaliyofanywa na Bunge la 11, liliondoa neno Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Kambi Rasmi ya Waliowachache Bungeni.
Katika nafasi hiyo, Ndugai ni mgombea pekee aliyejitokeza. Shughuli ya upigaji kura imemalizika na kura zinaendelea kuhesabiwa.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment