WAJUMBE wa Kamati ya Ukimwi, Manispaa ya Morogoro, wanajipanga kutoa elimu ya ujasiriamali, kwa makundi mbalimbali wakiwemo vijana. Anaandika Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Wameeleza, lengo ni kuwakuza kiuchumi pamoja na kusaidia kuepuka vishawishi vinavyosababisha maambukizi mpya ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) kila siku.
Hayo yalisemwa leo tarehe 14 Novemba 2019, na mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo, Joseph Mlay wakati akizungumza kwenye kikao cha kwanza cha maandalizi ya kilele cha wiki ya Ukimwi dunia – Desemba Mosi mwaka huu.
Mlay ambaye pia ni Mkurugenzi wa Shirika la Care Youth Foundation amesema, makundi mbalimbali wakiwemo vijana na wenye ulemavu, wamekuwa kwenye hatari ya maambukizi mara nyingi kutokana na kukosa fedha za kujikimu.
Amesema, endapo watazingatia na kuitumia vyema elimu hiyo ya ujasiliamali, itawasaidia kuwainua kiuchumi na kuwaepusha na vishawishi.
Michael Waluse, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, amewataka wajumbe kutambua kuwa, bado wana kazi kubwa ya kufanya, kuhakikisha kiwango cha maambukizi katika manispaa hiyo kinapungua kufuatia asilimia 4.5 ya maambukizi iliyopo kuwa sawa na asilimia 50.
Upendo Elias, Mratibu wa Ukimwi Manispaa ya Morogoro amesema, hali ya maambukizi hayo kwenye manispaa hiyo ni asilimia 4.5 kulingana na watu waliojitokeza kupima kwenye vituo vya afya.
Elias amesema, katika kilele cha Siku ya Ukimwi Duniani mwaka huu, wamejipanga kutoa elimu nasaha na upikaji wa virusi hivyo kwa wananchi wote wa manispaa hiyo.
Amesema, upimaji wa VVU utaenda sambamba na upimaji wa magonjwa ya Sukari na Saratani, pamoja na ukusanyaji damu salama kwa ajili ya wagonjwa wa dharura.
Siku ya Ukimwi Duniani huazimishwa Desemba Mosi kila mwaka, na kwa mwaka huu kitaifa yatafanyika jijini Mwanza.
Leave a comment