KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira, imependekeza kuwa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kipewe mamlaka kamili badala ya kuwa wakala wa Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akisoma maoni ya kamati kuhusu Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya mwaka 2022, leo Jumanne tarehe 1 Novemba, 2022, bungeni jijini Dodoma, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, David Kihenzile amesema hadhi ya TIC haiwezeshi mfumo Madhubuti wa kitaasisi kwaajili ya uratibu na uwezeshaji wa uwekezaji nchini.
“Kwa sababu hiyo, Kamati inapendekeza Kituo cha uwekezaji kipewe Mamlaka kamili badala ya kuendelea kuwa Wakala wa Serikali, lengo ni kukipa nguvu ya utekelezaji wa majukumu yake,” amesema Kihenzile.
Kamati inapendekeza pia kuwa baada ya Sheria hiyo kutungwa na Bunge ‘‘itafsiriwe katika Lugha ya Kiingereza ndani ya siku 30.
Sababu ni uhalisia wa Uwekezaji ambao kutokana na vivutio katika Muswada huu Wawekezaji wengi wanatarajiwa kutoka mataifa mbalimbali.”
Pia kamati imetoa maoni na mapendekezo ya mabadiliko ya baadhi ya vifungu ikiwemo Kifungu cha kwanza kuhusu Jina la sheria hiyo.
“Kamati inashauri Jina la Sheria lisomeke Sheria ya kuvutia na kulinda Uwekezaji Tanzania ya mwaka 2022,” amesema.
Aidha katika Kifungu cha 3 cha Tafasiri, Kamati imeshauri kuongezeke Maneno ‘ardhi’ na ‘Hakimiliki’ kwenye tafsiri ya neno ‘Mtaji’.
Leave a comment