KAMATI Kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo, jana tarehe 19 Juni 2021, iliuchambua uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita ya Tanzania, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumapili, tarehe 20 Juni 2021 na Salim Bimani, Katibu wa Habari, Uenezi, Mahusiano na Umma wa ACT-Wazalendo, akitangaza maazimio ya kikao cha kamati hiyo, kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya Bimani imesema, kamati hiyo ilijadili ufanisi wa Serikali ya Rais Samia, ikiwemo mageuzi aliyoyafanya katika nyanja mbalimbali, tangu alipoingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli.
Magufuli alifariki dunia akiwa madarakani, tarehe 17 Machi mwaka huu, katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu ya ugonjwa wa moyo. Mwili wake ulizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, tarehe 26 Machi 2021.
Taarifa ya Bimani imesema, kufuatia mageuzi yaliyofanywa na Rais Samia, kamati hiyo imeshauri yawekewe msingi wa kisheria, ili yawe endelevu.
“Kamati Kuu imejadili ufanisi wa Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais Samia. Imesisitiza mageuzi yanayofanywa kwenye nyanja mbalimbali tangu Serikali hiyo iingie madarakani, yawekewe msingi wa kisheria ili kuyafanya yawe yenye misingi madhubuti na endelevu,” imesema taarifa ya Bimani.
Pia, taarifa ya Bimani imesema kamati hiyo imeelekeza uongozi wa ACT-Wazalendo, ushirikiane na wadau wengine kudai katiba mpya, tume huru ya uchaguzi na mabadiliko ya Sheria ya Vyama vya Siasa nchini.
“Kwa kipekee kamati kuu imeelekeza chama kiendelee kupigania mabadiliko ya Sheria ya Vyama vya Siasa, ili vyama viendelee kifanya kazi kwa uhuru. Pia, imeelekeza chama kiendelee kuwa mstari wa mbele katika kupigania katiba mpya na tume huru ya uchaguzi. Kwa kuahirikiana na makundi mbalimbali ya kijamii, kama asasi za kiraia, viongozi wa dini, wanaharakati, wanazuoni na umma kwa ujumla,” imesema taarifa ya Bimani.
Tangu Rais Samia aingie madarakani, amefanya mageuzi katika utawala wa sheria, kwa kuhakikisha kesi za kubambikizwa zinafutwa, kupunguza mrundikano wa mahabusu pamoja na vyombo vinavyohusika na masuala ya mashtaka kupitia upya mienendo ya kesi zao.
Mageuzi hayo ya kisheria yaliwagusa Masheikh 18 wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI), waliofutiwa mashtaka ya ugaidi katika Kesi ya Jinai Na. 121/2021, iliyokuwa inawakabili kwenye Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam.
Masheikh hao walifutiwa mashtaka tarehe 15 Juni 2021 na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Silvester Mwakitalu, baada ya kubaini mashtaka hayo hayakuwa na nguvu kisheria.
Mageuzi mengine yaliyofanywa na Rais Samia, ni katika masuala ya uwekezaji, kwa kuhakikisha wizara na taasisi zinazosimamia sekta hiyo, zinaweka sera rafiki ili kuvutia wawekezaji. Huku kiongozi huyo akiwaita wawekezaji waliokimbilia nje ya nchi kwa sababu mbalimbali, warejee nchini, akiwahakikishia kulinda uwekezaji wao.
Pia, Rais Samia alifanya mabadiliko katika ukusanyaji maoayo na kodi, kwa kuondoa vikosi kazi (Task Force), vilivyoundwa kwa ajili ya ukusanyaji mapato, na kulirudisha jukumu hilo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Kiongozi huyo wa Tanzania, aliiagiza TRA iache kubambikizia watu kodi na kutotumia nguvu wakati wa ukusanyaji mapato, huku akiweka bayana msimamo wa Serikali yake, kwamba inahitaji ukusanyaji mapato halali kutoka kwa wananchi na si ya dhulma.
Leave a comment