IKIWA ni siku tatu tangu tukio la kupotea kwa msanii wa miondoko ya Hip Hop Ibrahim Mussa ‘Roma Mkatoliki’ na wenzake watatu Kamishna wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro amesema hali ya nchi kiusalama bado ni njema, anaandika Hamisi Mguta.
Kamanda Sirro amesema kuwa matukio ya watu kutekwa yameanza muda mrefu na kuwa tukio la kukamatwa kwa wasanii hao si kigezo cha watu kupatwa na taharuki na kusema hali ya kiusalama nchini ni mbaya.
“Hili ni tukio kama matukio mengine na hali ni ya kawaida sana huwezi ukasema hali ni mbaya kwasababu hawa vijana wametekwa,” amesema.
Wasanii Moni, Bin Laden, Emanuel na Roma walikamatwa Aprili 5 na watu wasiojulikana majira ya saa moja katika studio za Tongwe records zilizopo Masaki jijini Dar es Salaam, hadi sasa Jeshi la Polisi na vyombo mbalimbali vya usalama hakuna anayefahamu nani aliyewateka. ingawaje taarifa zisizokua na uhakika zinaeleza kuwa ameonekana kituo cha Polisi Oysterbay leo saa 7 mchana.
Kamishna Sirro amekiri kupokea taarifa za kutekwa kwa wasanii hao na kuahidi kulifanyia uchunguzi kubaini waliofanya tukio hilo.
“Tukio lilitokea tarehe 5 Aprili mwaka huu katika studio inayoitwa Tongwe records, ambapo inadaiwa kuwa ilifika gari aina ya Noah ambayo namba zake hazikusomeka yenye rangi ya Silva ikiwa na watu watano.
“Wakaingia kwa nguvu na kuchukua televisheni 1 aina ya Sony, Kumpyuta moja na kamera na kisha kuondoka na wasanii hao wanne, tumeunda timu yetu ya upelelezi ambayo inaendelea vizuri mpaka sasa,” amesema.
Sirro amesema jambo hilo limeshafika Polisi na ni vyema liachwe lishughulike na Polisi,
Hata hivyo jana uongozi wa mkoa wa Dar es Salaam uliahidi kuwa wasanii hao watakuwa wamepatikana kabla ya tarehe 9 Aprili- kesho Jumapili
Hata hivyo Sirro amesema, “mimi ni ofisa wa Polisi anayefanya kazi kwa kuzingatia taaluma, siwezi kusema ni lini wasanii watapatikana, Kama kuna kiongozi kasema, yeye ndio atakua na majibu ikifika kesho. Mimi simsemei.”
Kwa upande mwingine Kamishna Sirro ameshangazwa na kitendo cha wasanii kuungana na kufanya shinikizo juu ya jambo hilo na kusema, polisi wapo kisheria na wanafanya kazi kwa mujibu wa taratibu zao.
“Haya matukio yangekua ikitokea watu wameibiwa Kariakoo wote wanakutana wanatoa shinikizo ingekuwaje? Hii kazi tumepewa kwa mujibu wa Katiba kwahiyo tupeni muda,” amesema.
Leave a comment