LAZARO Mambosasa Kamanda wa Kanda Maalumu Dar es salaam amewataka wananchi wote pamoja na waandishi wa habari kumpa ushirikiano ili jamii iweze kuishi katika hali ya usalama na amani Anaandika Victoria Chance.
Ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam kwenye mkutano na waandishi wa habari alipozungumza ikiwa ni siku ya kwanza kuanza kazi katika kanda maalum.
Mambosasa amesema kuwa polisi wanaokamata raia kwa madai kuwa ni agizo kutoka juu hawajiamini na hapendi kuona wananchi wanaonewa.
“… Watanzania wote wako huru na uhuru huo siyo wa maombi, unatokana na haki za kibinadamu na siyo wa kuuchezea na sipo tayari kuona askari wakimnyanyasa mtu.”
“Hiyo amri ya kusema kwamba imetoka juu itakuwa siyo sahihi na ili kuondoa hilo nimetoa namba za simu ili mtu ahoji kwangu kwamba kamanda nakamatwa hapa naambiwa ni amri kutoka juu,” aliongeza.
Hivi karibuni wanasiasa akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wamekuwa wakikamatwa na maofisa wa polisi huku baadhi yao wakidaiwa kusema kwamba wametumwa na kupewa maagizo kutoka juu ili kuwakamata.
Akizungumzia makundi ya vijana kama wajulikano kama ‘panya road na roho saba’ Mambosasa ametaka ushirikiano kutoka kwa makamanda wengine, “Kwangu kwanza ni kukomesha uhalifu lakini sitokomesha nikiwa peke yangu nina makamanda wa mikoa mitatu ya Temeke, Kinondoni na Ilala hao mimi nitashirikiana nao.
Mambosasa ameteuliwa wiki iliyopita na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro kuwa Kamanda wa Kanda Maalumu Dar es Salaam nafasi iliyokuwa inashikiliwa na Lucas Mkondya.
Leave a comment