WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Angellah Kairuki amesema wakurugenzi wa halmashauri ambao watashindwa kufikia malengo ya ukusanyaji mapato, ‘watapigwa chini’. Anaripoti Safina Sarwatt, Arusha…(endelea).
Kairuki ametoa kauli hiyo leo Alhamisi wakati akifunga Mkutano Mkuu wa 37 wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) uliofanyika jijini Arusha.
Amesema baadhi ya halmashauri nchini zikiongozwa na Jiji la Dar es Salaam, Manispaa ya Kinondoni na Ubungo, wameshindwa kutoa leseni za biashara kwa wahitaji jambo hilo linaweza kukosesha mapato kwa halmashauri.
“Tutapataje pesa kama hatutoi leseni. Halmashauri haiwezi kupata mapato kama hakuna watu wanaofanya biashara na baadhi ya halmashauri ikiwemo Jiji la Dar es Salaam hawatoi leseni kwa baadhi ya wafanyabiashara wanaohitaji leseni hizo. “Hivyo Mkurugenzi ambaye atashindwa kufikia malengo ya ukusanyaji mapato hatavumilika,” amesema.
Amesema, baadhi ya halmashauri hazipeleki benki fedha mbichi jambo hilo linasababisha halmashauri kupata hati chafu ikiwemo hoja za ukaguzi.
Kairuki amewataka wakuu wa mikoa na wilaya kufanya kazi na madiwani kwa mahusiano mazuri ili fedha zinazopelekwa kwenye halmashauri zinasimamiwa na watu wanaoshirikiana, huku kila mmoja akiheshimu mipaka na wengine.
Akizugumzia mashine za ukusanyaji mapato (Posi) amesema kuwa halmashauri kumi zimeonekana kuzima posi kwa muda mrefu ikiwemo Mbeya Jiji – posi 124, Dodoma Jiji- posi 121, Temeke – posi 95, Kinondoni – posi 88, Tunduma – posi 84, Iramba – posi 81, Dar es salaam Jiji – posi 77, Mbarali – posi 74, Makete – posi 72 na Muleba – posi 72.
“Hizi ni halmashauri 10 ni chache ambazo nimezitaja na siyo kwamba wengine hawazimi posi hivyo basi naomba niwaambie kwamba kila mmoja awajibike kwasababu suala hili halitavumilika nendeni mkajipange,” amesema Kairuki.
Leave a comment