Akihubiri parokiani hapo, katika misa ya kuuaga mwili wa Flugence Mapunda, aliyekuwa kada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) leo tarehe 9 Oktoba 2019, Padri Sabuni amesema tunabaguana.
Padri Sabuni ametoa wito kwa jamii, kutii amri ya kupendana akisema kwamba, dunia si ya watu, bali wanapita.
“Bwana Yesu alituachia amri kuu mbili, amri ya kwanza kuu ni mpende Mungu wako, amri ya pili mpende jirani yako. Lakini tunabaguana.
“Nikiuliza leo hii unampenda jirani yako, wako wengine watasema huyu nampenda huyu ni adui yangu. Wanangu mkeshe katika upendo na kusaidiana, hii dunia si ya kwetu,” amesema Padri Sabuni.
Padri Sabuni ameihimiza jamii kutenda yaliyo mema ili kuitafuta huruma ya Mungu, kama marehemu Mwanacotide alivyotenda yaliyo mema enzi za uhai wake.
“Tendeni matendo mema. Hakuna mtu mkamilifu, sisi sote ni wa dhambi. Tutafute huruma ya Mungu. Flugence ( MwanaCotide) aliwapenda watu, aliwaongoza watu. Ndio maana kwenye chama chake wanasikitika watazibaje pengo lake,” amesema Padri Sabuni.
MwanaCotide alifariki dunia tarehe 6 Oltoba 2019, katila Hospitali ya St. Monica jijini Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu. Mwili wa MwanaCotide unatarajiwa kuzikwa kwao Lituhi, wilayani Nyasa, Ruvuma.
Leave a comment