AFISA wa Zamani wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), Kevin Mallory (62) amefungwa miaka 20 jela kwa kosa la kutoa siri za taifa hilo kwa wakala wa China. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Katika kesi iliyokuwa ina mkabili kwenye Mahakama ya Idara ya Haki, Mallory alikutwa na hatia ya makosa kadhaa ya upelelezi, kutokana na kachero huyo kuwa na wadhifa mkubwa katika idara ya upelelezi pamoja na kuwa na nafasi nzuri ya kuona nyaraka nyeti za Marekani.
Mallory alihukumiwa kwa kuuza siri za Marekani kwa China kwa gharama ya kiasi cha dola 25,000. Ushihidi uliotumika katika kumtia hatiani, ni wa video inayomuonesha akichapisha kwa siri nyaraka zilizowekwa kwenye memori, katika ofisi ya posta.
Pia, ushahidi mwingine ulimuonesha Mallory akisafiri kutoka Marekani kuelekea mjini Shanghai China kwa ajili ya kukutana na wakala wa China katika kipindi cha mwezi Machi na Aprili mwaka 2017.
Mwanasheria wa Marekani, Zachary Terwilliger katika tamko lake amesema Mallory si kwamba ameiweka nchi hiyo kwenye hatari kubwa peke yake, bali amehatarisha usalama wa maisha ya raia wa Marekani.
Terwilliger amesema hukumu ya Mallory ni ujumbe kwa mtu yeyote anayepanga kuvunja uaminifu kwa umma na kuhatarisha usalama wa Marekani, kwa kuwa wataendelea kufuatilia changamoto hiyo kwa ajili ya kuimarisha usalama wa taifa hilo.
Mallory aliwahi kuwa Afisa wa CIA na Afisa wa Upelelezi wa Wakala wa Upelelezi wa Masuala ya Intelijensia Marekani (DIA).
Leave a comment