Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), limetoa ufafanuzi kuhusu vitendo vya rushwa, ulaghai na utapeli vinavyofanywa na baadhi ya watu wasio waaminifu, wakiwaahidi watu mbalimbali kwamba watawasaidia kupata nafasi ya kuandikishwa katika nafasi za ajira zilizotangazwa na jeshi hilo. Anaripoti Rhoda Kanuti… (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 30 Novemba, 2021 jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa JWTZ, Luteni Kanali Gaudentius Ilonda amesema matapeli hao wameenda mbali zaidi na kutumia jina la mkuu wa majeshi.
Amesema matapeli hao wanadai kuwa Mkuu huyo wa majeshi ndiye aliyewatuma kukusanya fedha ili wapate nafasi ya kuandikishwa, jambo ambalo si la kweli.
Aidha, amewataka wananchi kutoa taarifa haraka endapo watakutana na watu wa aina hiyo, na kusisitiza kwamba jeshi halina utaratibu wa kuwatoza watu fedha ili wapate nafasi ya kujiandikisha na kwamba wanaofanya vitendo hivyo ni matapeli.
Aidha, amewaonya baadhi ya wazazi ambao wameanza kuwatafuta viongozi serikali na kuwaomba vijana wao wajiunge na jeshi hilo kwa visingizio mbalimbali.
“Jeshi haliandikishi vijana kwa kutafuta pesa bali ni jeshi ambalo linafuata sheria na sifa kwa kijana.
Leave a comment