IKIWA imebaki siku mbili Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) litimize miaka 54 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964, limetangaza mafanikio yake ikiwemo kuimarisha usalama wa nchi na nchi jirani. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 29 Agosti, 2018 , Kanali Ramadhan Dogoli, Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano JWTZ, amesema jeshi hilo limepongezwa na Umoja wa Mataifa (UN) kutokana na mchango wake katika kuimarisha usalama na ulinzi katika nchi zenye migogoro hasa Sudani Kusini, DR Kongo na Lebanoni.
Katika hatua nyingine, Kanali Dogoli amesema JWTZ itaendelea kuimarisha ulinzi na usalama nchi na kuwaahidi Watanzania kwamba litaendelea kuwa imara pasina kutetereka.
Kuelekea kilele cha siku ya maadhimisho ya miaka 54 ya JWTZ, Kanali Dogoli amesema jeshi hilo linafanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kufanya usafi, ambapo amewataka watanzania kuungana na jeshi hilo katika kufanya usafi kwenye maeneo yao.
“Katika maadhimisho ya mwaka huu, Jeshi letu limeanza kufanya shughuli mbalimbali za usafi kwenye maeneo ya kambi zote za jeshi, pamoja na kufanya michezo mbalimbali vikosini ambapo michezo mingine itakuwa baina ya timu za jeshi na zile za uraiani,” amesema Kanali Dogoli.
Leave a comment