KUELEKEA maandalizi ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania imeiomba serikali kuunda Tume Huru ya Uchaguzi ili kuleta haki na usawa katika uchaguzi huo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Wito huo umetolewa na Taasisi hiyo kupitia waraka ulilotolewa kamati yake kuu ya Siasa ya Shura ya Maimamu leo tarehe 12 Agosti 2019.
Waraka huo uliotolewa na Sheikh Ponda Issa Ponda, Katibu Mkuu Kamati Kuu ya Siasa ya Shura ya Maimamu Tanzania umeeleza kuwa, serikali ina wajibu kuhakikisha usawa na haki vinatendeka katika uchaguzi huo.
“Kwa upande wa serikali matarajio ya Waislamu Tanzania ni kuwa Serikali itakubali kuundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao mwaka 2020,” unaeleza waraka huo.
Kuhusu uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwaka huu, jumuiya hiyo imetoa wito kwa serikali kuhakikisha kwamba unafanyika kwa haki na amani.
“Hata hivyo methali inasema “chenye upungufu hakitupwi chote”. Kwa lugha nyingine katika kipindi hiki cha mpito watu watashiriki uchaguzi. Kwa muktadha huo ni wajibu wa serikali kuhakikisha usawa na haki vinatendeka katika jambo hili kubwa la haki ya watanzania,” .
Pia, Jumuiya hiyo imemtaka Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungu kutumia hekima na busara kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa kwa wananchi na wanasiasa ili isiwe
“Hivyo tunatoa wito kwa Msajili wa vyama vya siasa kutumia hekima, busara na kuzingatia misingi ya haki na usawa kwa wananchi na wanasiasa kwa ujumla ili asiwe dara la kuharibu kabisa kiasi cha amani na utulivu kilichopo,’ unaeleza waraka huo.
Wakati huo huo, Jumuiya hiyo imewahimiza wananchi kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa ikiwemo kujiandikisha katika daftari la wapiga kura.
“Ni muhimu tuelewe kuwa serikali hizi za Mitaa, vijiji, vitongoji ni mamlaka muhimu sana yenye mguso mkubwa katika maisha ya watu, mali zao, uchumi na utamaduni wao, pengine kuliko hata serikali kuu au Bunge. Kwa namna hiyo uongozi wake si jambo la kupuuzwa,”
“Shura ya Maimamu kupitia Waraka huu inawahamasisha watanzania Waislamu na wananchi kwa ujumla kushiriki uchaguzi kwa umakini. Watu wajiandikishe katika daftari la wapiga kura na walinde kura. Wawachague wagombea kwa vigezo muhimu na umakini wa vyama vyao. Ifahamike kuwa wagombea hao ndio watakaokuwa viongozi wenye maamuzi na watekelezaji wa mambo yenu,” unaeleza waraka huo.
Leave a comment