JUMUIYA YA Kikristo Tanzania (CCT), imezichambua siku 100 za uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, na kutaja mambo matano yaliyong’arisha siku hizo.Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia aliyeingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, alitimiza siku 100 za uongozi wake katika Serikali ya Awamu ya Sita, tarehe 27 Juni mwaka huu.
Magufuli alifariki dunia kwa ugonjwa wa moyo, tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, na mwili wake ulizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, tarehe 26 Machi mwaka huu.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa CCT, leo tarehe 8 Julai 2021 mkoani Morogoro na Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Askofu Alinikisya Cheyo, amesema Rais Samia imejipambanua kama rais anayesimamia misingi ya utawala bora na haki za binadamu.
“Takribani siku 100 zimepita tangu uwe rais wetu, tunakupongeza kwa mambo mazuri umeweza fanya, umeendelea kudumisha amani na utulivu wa nchi, umoja wa kitaifa. Umejiambanua kwa hakika ni rais wa Watanzania wote unasimamia misingi ya utawala na bora haki za binadamu,” amesema Cheyo.
Cheyo amesema, katika siku hizo, Rais Samia amefanikiwa kufungua milango ya kiuchumi, kuimarisha diplomasia, kuboresha mazingira ya ulipaji kodi na uwekezaji.
“Umefungua milango zaidi ya kuimarisha uchumi wa nchi yetu, tumeshuhudia Serikali unayoiongoza ikiongeza mishahara kwa watumishi, umeweka mazingira rafiki kwa watu kulipa kodi na sisi viongozi wa dini tulikuwa tunaminywa lakini asante sana, mazingira yamekuwa rafiki bila kuathiri utoaji huduma,” amesema Askofu Cheyo na kuongeza:
“Katika muda mfupi wa uongozi wako, tumeona Serikali yako ikiweka mazingira salama ya wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza nchini. Tunakupongeza kwa kuimarisha diplomasia kwa nchi marafiki na kimataifa, ni muhimu sana kwa ustawi wa nchi yetu.”
Leave a comment