DAKTARI John Magufuli, Rais wa Tanzania leo tarehe 15 Agosti 2019, amefanya mazungumzo na Cyril Ramaphosa, Rais wa Afrika Kusini, kuhusu ushirikiano wa mataifa hayo katika sekta ya biashara, uwekezaji, afya, miundombinu, ulinzi na usalama. Anaripoti Hamisi Mguta … (endelea).
Mazungumzo hayo yamefanyika Ikulu jijini Dar es Salaam, siku moja baada ya Rais Ramaphosa kuwasili nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi ya siku mbili, ikiwa ni pamoja na kuhudhuria mkutano wa wakuu wa nchi mwanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC.
Rais Magufuli ameeleza kwamba, mazungumzo hayo yalijikita katika namna ya kutumia uhusiano wa mataifa hayo mawili kuimarisha uchumi wa Tanzania na Afrika Kusini.
“Kwanza tulifanya mazungumzo ya faragha na kisha tukafanya mazungumzo rasmi, mazungumzo yetu kwa ujumla yalijikita katika kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi. Kama mjuavyo Afrika Kusini ni nchi yenye uchumi mkubwa barani Afrika inashika nafasi ya 2 baada ya Nigeria, na ni nchi pekee Afrika iliyopo kwenye kundi la nchi 20 tajiri duniani ‘G 20’,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli ametaja masuala ambayo amekubaliana na Rais Ramaphosa kuyafanyia kazi kwa pamoja, hasa uboreshaji wa mazingira ya biashara na uwekezaji baina ya Tanzania na Afrika Kusini, ikiwemo uondoshaji utitiri wa kodi, usimamizi wa masuala ya biashara na uwekezaji pamoja na uanzishwaji wa viwanda.
Suala lingine ni ushirikiano katika sekta ya madini, ambapo wakuu hao wa nchi wamekubaliana kubadilishana uzoefu na utaalamu wa usimamizi wa sekta hiyo pamoja na wawekezaji wa Afrika Kusini kujenga viwanda vya kuchakata na kuongeza thamani madini hapa nchini.
“Kuhusu madini eneo hili ni muhimu kushirikiana hususan katika kubadilishana uzoefu na utaalamu wa usimamaizi wa sekta hii, aidha nimewakaribisha wawekezaji kutoka Afrika Kusini kuja kujenga viwanda vya kuchakata na kuongeza thamani ya madini yetu hapa nchini,” amesema Rais Magufuli.
Licha ya hayo, Rais Magufuli amemuahidi Rais Ramaphosa kushirikiana na serikali yake katika masuala ya afya, na kumhakikishia kwamba Tanzania itanunua dawa kutoka katika viwanda vinavyozalisha dawa nchini mwake.
“Katika bajeti yetu ya kununulia madawa kwa mwaka huwa zaidi ya bilioni 270, lakini karibu asilimia 98 ya fedha hizi hutumika kununua dawa kutoka nje, tumewakaribisha wenzetu, tutanunua hapa hapa kwa njia hiyo madawa yatakua bei rahisi,” ameahidi Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli amesema amekubaliana na Rais Ramaphosa kuwa watalaamu wa afya wa Tanzania watakwenda Afrika Kusini kwa ajili ya kujengewa uwezo, hususan wataalamu wa dawa za usingizi na huduma za wagonjwa mahututi na dharula.
“Lakini kitu kingine tutabadilishana utaalamu ambao upo kati ya Tanzania na Afrika Kusini. Katika eneo la kujenga uwezo wa watalaamu wetu wa dawa za usingizi na huduma za magonjwa mahututi na dharula ili tuweze kushirikiana kwa pamoja,” amesema Rais Magufuli.
Pia Rais Magufuli amesema katika mazungumzo yao amekubaliana na Rais Ramaphosa kubadilishana ujuzi na utalaamu katika masuala ya ulinzi na usalama.
“Lingine ni suala la ulinzi, tumekubaliana tuimarishe, na nimemuomba baadhi ya watalaamu wetu wa masuala ya ulinzi waende wakapate mafunzo kule na amekubali,” amesema Rais Magufuli.
Rais Ramaphosa amemhakikishia Rais Magufuli ya kwamba waliyokubaliana katika mazungumzo hayo yatafanyiwa kazi na serikali yake kwa masilahi ya pande zote mbili.
Aidha, Rais Ramaphosa amesema serikali yake kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania itaimarisha ushirikiano katika sekta ya nishati, mafuta na miundombinu.
“Naomba nichukue fursa hii kuwapongeza kwa mapokezi mazuri, tulifanya mazungumzo mafupi. Katika mazungumzo yetu, tulipata fursa ya kujadili mambo yanayohusu nchi zetu.
“Ikiwemo Kuimarisha mahusiano ya watu, kuhakikisha tuna uwekezaji kati ya nchi zetu, maendeleo ya miundombinu na ushirikiano katika sekta ya nishati na mafuta,” amesema Rais Ramaphosa.
Leave a comment