RAIS John Magufuli amemuagiza Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Profesa Makame Mbarawa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Prof. Kitila Mkumbo kufanya uchunguzi kuhusu sababu za kukwama kwa mradi wa maji uliochini ya Mamlaka ya Maji Musoma (MUWASA) na kutekelezwa na Kampuni ya Ujenzi ya Nyakirang’anyi. Anaripoti Regina Kelvin…(endelea).
Rais Magufuli ametoa agizo hilo leo katika mkutano wake na wananchi wa Wilaya ya Bunda, ambapo amesema Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere akitokea leo atashangazwa kusikia mradi huo haujakamilika kutokana na kuanza kutekelezwa miaka nane iliyopita.
“…Wanabebana, si ndio nasema wataachiana, naomba hilo mniachie hilo nitalibeba mwenyewe, kama mkandarasi ni mshenzi na mi ni mshenzi zaidi, kama kutumbua watu nitatumbua, kufukuza nitafukuza ilimradi mradi wa maji ufanikiwe,” amesema Rais Magufuli.
Hatua hiyo ya Rais Magufuli imekuja baada ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima kubainisha kuwa mkandarasi huyo hana dalili za kumaliza ujenzi wa mradi huo na kwamba alimshauri aliyekuwa Waziri wa Maji, Isaac Kamwele kuuvunja mkataba wa ujenzi huo.
“Mradi wa maji wa Bunda tuliambiwa umekamilika kwa asilimia 58 tulipokwenda tuliona haujakamilika kwa asilimia hizo, tenki lina zaidi ya miaka 10 halijafanya kazi, mkandarasi na mkurugenzi amechukuliwa hatua na kuwekwa ndani. Sidhani kama anaweza kuumaliza huo mkataba na alipokuja Kamwele tulimsihi tuvunje mkataba na atafutwe mkandarasi mwengine, “ amesema Malima.
Kabla ya hapo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bunda, Simona Mayaya alimuomba Rais Magufuli kuingilia kati tatizo la ukosefu wa maji linaloukabili mji huo.
Leave a comment