RAIS John Magufuli amewataka viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutobweteka kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na viongozi wa chama hicho wa mikoa na wilaya leo tarehe 24 Januari 2020, jijini Dar es Salaam Rais Magufuli amewasihi kutopuuza nguvu ya vyama vya upinzani, kwa kuwa wamebadilika.
Rais Magufuli amesema, washindani wa CCM wa leo sio wa miaka ya nyuma, kwani wamebadilika na wanabuni mikakati mingi, inayojulikana na isiyojulikana, katika kuhakikisha wanapata ushindi kwenye uchaguzi huo.
“CCM ya leo sio ya miaka ya nyuma lakini lazima tutambue pia, washindani wetu wa leo sio wa miaka ya nyuma, nao wamebadilika. Wanabuni mikakati mingi, mikakati yao mingine ya hadharani lakini mingine ya siri, tusibweteke,” amesisitiza Rais Magufuli.
Rais Magufuli ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, amewataka viongozi na wanachama wa chama hicho, kujiandaa vyema katika kushiriki uchaguzi huo.
“Lazima kama chama tujitathimini tuwe na uhakika wa maandalizi halisi katika uchaguzi, ni lazima tufanye hivyo kwa sababu pamekuwa na mabadiliko mengi. Na chama chetu kimebadilika, kwa hiyo ni vyema tukajidhatiti na kujiweka katika hali ya ushindi,” ameeleza Rais Magufuli.
Leave a comment